Tayari watafiti wengi wamekubali ya kwamba kuna usalama mkubwa kwenye app ya Telegram kwenye suala zima la data za watumiaji. Telegram wanaenda hatua zaidi katika suala hili.
Kuanzia sasa watu wanaotumia toleo jipya la Telegram wanauweza wa kufuta si ujumbe waliotuma wao tuu kwenye mazungumzo (chat), bali wanaweza kufuta chati nzima upande wao na kwenye upande wa mtu waliokuwa wanachati naye.
Kwa muda wa takribani miaka miwili sasa watumiaji wa app ya kuchati ya Telegram wamekuwa na uwezo wa kufuta (unsend) ujumbe waliotuma kwenye chat ndani ya masaa 48 baada ya kutuma – yaani kama umekosea basi unaweza kuufuta ujumbe huo kwako na kwenye simu ya uliyemtumia ndani ya masaa 48.
Kuanzia sasa suala la muda halijalishi tena, pia haijalishi kama ni ujumbe uliotuma wewe au uliotumiwa na uliyekuwa unachati naye – utaweza kufuta mazungumzo (chati) nzima upande wako na wa kwa yule uliyekuwa unawasiliana naye.
Bwana Pavel Durov ambaye ni mwanzilishi wa huduma ya kuchati ya Telegram anasema wamefanya hivi kuokoa watumiaji wake isije ikatokea mazungumzo waliyofanya na mtu miaka kadhaa nyuma kuja kutumiwa kuwaharibia maisha mbeleni. Na kwa kufanya hivi si watu binafsi tuu watanufaika na hili bali ata waandishi wa habari ambao huwa wanapewa taarifa nyeti na wavujishaji habari, upande wote utakuwa na amani wakijua watafuta mazungumzo hayo muda wowote watakaotaka.