Wakati watanzania wakiwa wanaendelea kukumbushwa kuhusu kwenda kusajili upya kadi zao za simu sasa imeshajulikana tamati ya zoezi hilo.
Zoezi la usajili wa kadi za simu kwa njia ya alama za vidole (fingerprint) linalotarajiwa kuanza Mei 1 2019 limeleezwa kwamba tamati yake itakuwa mwezi Disemba 31, 2019. Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Atashasta Nditiye Bungeni kwamba mwisho wa usajili wa kadi za simu kwa njia ya kutumia alama za vidole na kitambulisho cha utaifa au Namba za NIDA ni tarehe 31/12/2019.
Aidha, ifikapo tarehe hiyo line ambazo hazijasajiliwa zitafungwa na TCRA kutumika mpaka zitakaposajiliwa. Kadhalika, Mhe. Nditiye amesema mwezi Septemba watafanya angalizo la kujua wangapi wamesajili na changamoto zipi zilizojitokeza kwenye zoezi hilo. Takwimu zilizopo Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia ofisi za NIDA ni kwamba wananchi walio na namba za NIDA ni milioni 16.
Ufafanuzi ni kwamba zoezi hili litahusisha wenye vitambulisho vya Taifa na wale ambao bado hawajapata vitambulisho lakini wana namba za NIDA. Namba ya NIDA raia anaipata pale anapoanza mchakato wa kupata kitambulisho baada ya kujaza fomu husika kutoka NIDA.
Kwa ambaye ameanza mchakato na hakumbuki namba yake basi anaweza kupata namba yake kwa njia ya simu kwa kutumia menu hii *152*00# kisha utachagua namba 3, halafu chagua namba 2 na baada ya hapo utaingiza majina yako matatu iliyojaza katika fomu za NIDA, kisha utabonyeza kukubali. Baada ya muda mfupi utapata majibu ya namba yako ya NIDA. Njia hiyo ni lazima uwe na salio lisilopungua Tsh. 100 vinginevyo ni kwenda kwenye ofisi za NIDA zilizo karibu nawe.