Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, TCRA imetoa tangazo kwa wateja wote wanaotumia line za simu za makampuni ya mawasiliano kwamba kuanzia mwezi Mei mosi, 2019, usajili wa kadi za simu utakuwa kwa njia ya alama za vidole (fingerprint).
Sambamba na usajili huo wa alama za vidole pia mteja atatakiwa kuwa na kitambulisho cha Taifa au namba ya kitambulisho chake cha taifa kutoka NIDA iwapo bado hakijatoka; zoezi hili litawahusu wateja wote ambao kadi zao za simu zilisajiliwa kwa mfumo wa zamani.
Usajili huu wa Alama za vidole umekuja kufuatia matukio mengi ya uhalifu wa kutumia line za simu ambazo zina usajili fake na kutokuwa na taarifa rasmi zinazofahamika. Awali usajili wa line za simu ulitambua vitambulisho kadhaa ikiwemo hati ya kusafiria (passport), kitambulisho cha uraia, kazi/shule/chuo, benki, barua ya utambulisho kutoka serikali za mitaa na Vitambulisho vingine vinavyotolewa na mamlaka mbalimbali zinazotambulika kisheria.
Mwezi Agosti mwaka jana serikali ya Tanzania ilitangaza kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Mamlaka ya Vitambulisho Tanzania (NIDA), kuja na mpango wa usajili wa kadi za simu kwa kutumia alama za vidole ili kukomesha umiliki wa kadi za simu usiokuwa na usajili wenye taarifa makini zinazopelekea mtu kufanya uhalifu bila ya kufahamika.
Pia ilitangazwa kwa mtu atakayetaka kusajili kadi ya simu zaidi ya moja kwa kampuni moja ya simu atalazimika kujaza fomu maalumu ya kujieleza kwanini anahitaji line zaidi ya moja.