Kuna simu janja nyingi sana sokoni lakini kuna bidhaa kutoka makampuni fulani ambayo wakati fulani yalikosa umaarufu kutokana na ushindani ingawa kwa miaka ya karibuni mambo ni tofauti na kwa leo nazungumzia Motorola ambapo siku hizi simu janja zake zinaitwa kifupi tuu mathalani Moto Z4.
Katika soko la ushindani Motorola bado wanajitahidi kutoa simu janja ambazo zinavutia kulingana na mwenendo wa teknolojia ili kuweza kujidhatiti na katika siku za karibuni rununu (simu janja) amabayo inaongelewa sana kutoka kwao ni “Moto Z” toleo la nne ambayo mpaka hivi sasa kwa mujibu wa vyanzo ya kuaminika baadhi ya sifa za zimeshajulikana:
Kipuri mama. Simu husika inaelezwa kuwa na Snapdragon 675 SoC ikiwa ni moja ya vipuri mama ambavyo vina nguvu na kufanikisha ufanisi wa simu ambao utachagizwa na GB 6 za RAM.
Muonekano. Kwa mbele kabisa utakaribishwa na uwazi mdogo kwenye kamera ya mbele mithili ya tone la maji ikiwa na kioo aina ya OLED chenye urefu wa inchi 6.4. Kwa nyuma kuna kamera kama kawaida, chini kidogo utakutana na nembo ya kampuni husika+spika zilizopo chini kabisa karibu na mwisho wa simu, upande wa kulia ni vitufe vya kuongeza/kupungza sauti na kuzima/kuwasha simu. Kwa upande wa juu utakutana na sehemu ya kuchomeka kadi ya simu, spika, kipaza sauti (cha pili) kinachowezesha ukiongea na simu uweze kusikika upande wa pili. kwa chini kuna kitufe cha kuchomekea spika za masikioni na sehemu ya kuchomeka kimemeshi (USB-C).
Kamera. Simu janja ya Moto Z toleo la nne lina kamera moja nyuma yenye MP 48 ikiwa ndio kamera kuu halafu kwa mbele kwa ile ambayo ni mahususi kwa kujipiga mwenyewe ina MP 25.
Uwezo wa betri. Betri lake limeelezwa kuwa na 3600mAh ambapo mbali na hili pia ipo teknolojia cha kuchaji haraka (TurboCharge). Vilevile, itakuwa ni simu ambayo ina teknolojia ya kisasa kwa simu za Motorola inafahamika 5G Moto Mod. Unafikiri haitakuwa na teknolojia ya kutumia alama ya kidole? La hasha! Ulinzi/teknoljia hiyo imewekwa ndani ya kioo cha simu.
Simu hii haipo mbali sana kuzinduliwa pengine ndani ya mwezi/miezi nichache ijayo tukaiona na kwa taarifa za awali huenda ikauzwa kwa karibu $400|zaidi ya Tsh. 920,000 kwa bei ya ughaibuni.
Vyanzo: GSMArena, Phone Arena