Moja kati ya simu janja ambazo hazina siku nyingi kuzinduliwa na sifa zake kujulikana kinagaubaga ni Tecno Spark 7 ambapo zina wateja wengi hasa barani Afrika.
Katika kuangaza kwangu huku na kule nikakutana na taarifa kuhusu Tecno Spark 7 ambapo kwa mujibu wa taarifa ni kwamba itatoka Aprili 9 ya mwaka huu na mpaka sasa hizi ndio sifa ambazo zimeweza kufahamika; kimsingi ndio zinazofanya mtu aweze kusema rununu husika ni ya kawaida au la!
Muonekano/Kioo
Hapa kwa haraka haraka simu hii ina kioo chenye urefu wa inchi 6.8 ambacho kina sifa ya ung’avu wa hali ya juu uliozidi kawaida, kwenye kamera ya mbele pameingia ndani kiogo mithili ya tone la maji bila kusahau ufanisi wake unaongozwa na Helio G70 SoC ikisimama kama kipuri mama.
Kamera/Memori
Katika kipengele hiki simu hii ina kamera 2 nyuma na moja mbele ikinakshiwa taa mbili(2) zinazofanya picha ama picha mnato kuonekana vyema nyakati za usiku au sehemu ambazo zina mwanga hafifu. Upande wa nyuma ipo taa moja pia pamoja na teknolojia ya kutumia alama ya kidole. Kwenye upande wa memori RAM yake itaanzia GB 4.
Uwezo wa betri+Mengineyo
Kwa maoni yangu sehemu ambayo kampuni nyingi inavutia watu/wateja ni kwenye kipengele cha uwezo wa betri na Tecno Spark 7 inaelezwa kuwa na 6000mAh (ina uwezo wa kuduma na chaji kwa siku 41 iwapo itatumia kwa kupiga/kupokea simu tu) bila kusahau teknolojia ya kuchaji haraka, inatumia USB-C, sehemu ya kuchomeka spika za masikioni ipo na inapatikana katika rangi tatu taofauti-Bluu, Nyeusi na Kijani.
Ingawa ni kwa uchache lakini mengi zaidi yatafamika mara baada ya uzinduzi wake kufanyika siku chache zijazo. TeknoKona kama kawaida yetu tukaona ni vyema tulete mbele cha macho yako japo kwa uchache wake kuhusu makala hii. Usiache kutufuatilia kila inapoitwa leo.
Vyanzo: GSMArena, Mitandao mbalimbali.
One Comment