Watu wengi duniani wameshajua hatima ya kompyuta zao iwapo zinafaa kuwekwa Windows 11 au la! Na hii imetokana na urahisi wa teknolojia ambayo itakupa jibu ndani ya sekunde chache tuu.
Ingawa Microsoft wamefungua milango kwa kompyuta hata zile za zamani kuweza kutumia Windows 11 lakini pengine ni vyema tukafikiria mara mbili kabla ya kulazimisha kutumia programu hiyo endeshi ilihali tukifahamu fika kuwa itatutesa tuu.
Kwenye huu ulimwengu wa teknolojia na vifaa vya kidijiti kwa mapana yake suala zima la kushusha masasisho ni kitu muhimu sana katika kuhakikisha ufanisi lakini usalama wa vitu vyertu. Sasa kwa mujibu wa habari zilizopo ni kwamba zile kompyuta ambazo zitatumia/zinatumia Windows 11 lakini hazijakidhi vigezo basi huenda zisipokee masasisho yoyote kutoka kwa Microsoft.
Sasa kwanini Microsoft inaruhusu “Kompyuta za zamani” kuwekwa Windows 11?
Microsoft wamesema wanaruhusu kompyuta za zamani kutumia Windows kwa lengo la kusaidia biashara yao ili kujua programu hiyo endeshi inavutia/inachukiza kiasi gani kulingana na kompyuta ambapo inatumia Windows 11.
TeknoKona tunashauri iwapo unajua fika kuwa kompyuta yako haina uwezo wa kutumia Windows 11 basi ni vyema ukatulia na Windows 10 huku ukihakikisha inapokea masasisho na kuyapakua kwani ni muhimu sana kwa uhai wa vifaa vyetu.
Vyanzo: Engadget, mitandao mbalimbali
No Comment! Be the first one.