Wakati simu mbalimbali zimeshaanza kupata masasisho ya Android 11, tayari Google wanafanyia kazi toleo la Android 12. Kuna maboresho mbalimbali makubwa yashaanza kuonekana kwenye utengenezaji wa toleo hilo lijalo la Android.
Toleo la kwanza rasmi la majaribio ya Android 12 Beta linategemewa kuanza kupatikana kuanzia mwezi wa tano, wakati kukamilika kwake kunategemewa mwezi wa tisa. Kama kawaida likikamilika litaanza kwanza kupatikana kwa simu za Google Pixels kabla ya kuanza kufika kwa simu za watengenezaji wengine.
Maboresho gani yameanza kuonekana katika matoleo ya utengenezaji Android 12 (Toleo la AOSP)?
>Itakuwa rahisi zaidi masoko mengine ya apps kuwekwa na kufanya kazi
Google wamefungua uruhusu zaidi wa masoko mengine ya apps nje ya Google Play Store, ila lazima apps hizo zifuate mifumo ya kiusalama ya malipo ya Google Play.
>Kurahisishwa kwa mifumo ya kusasisha programu endeshaji
Kwa muda mrefu simu za watengenezaji wengine kama vile Samsung na wengine wengi zimekuwa zikichukua muda mrefu sana kupata masasisho muhimu kutokana na Google kuwategemea watengenezaji hao wa simu kutuma masasisho hayo. Kwenye Android 12 Google wametengeneza mfumo mpya wa masasisho kupitia app ya Google PlayStore. Hivyo kuna masasisho mbalimbali muhimu ya programu endeshaji yataweza kutumwa moja kwa moja na Google kwenda simu za Android za watengenezaji wengine bila kuleta matatizo yeyote.
>Uwezo wa kuzuia huduma za Intaneti kwa baadhi ya apps
Kuna uwezo wa kupumzisha huduma ya intaneti kwa apps zote ambazo zimepakuliwa na mtumiaji. Ingawa kwa sasa inaonesha kuna apps ambazo zitaweza kutuma notification tuu, ila uwezo wa intaneti kamili utabaki kwenye apps zilizokuja na simu tuu – system apps. Uhakika kamili wa jinsi mfumo huu utaweza kufanya kazi tutaufahamu kufikia mwezi wa tano.
>Uwezo wa kushare nywila/password ya WiFi kwa urahisi
Kwa watumiaji wa Android 11 watakuwa wanafahamu ya kwamba kwa sasa simu za Android zinauwezo wa kutuma mafaili kwenda kwenye simu nyingine kwa urahisi kupitia huduma ya Nearby Share – teknolojia inayowezesha kutuma mafaili makubwa na madogo kwa uharaka kutoka simu moja ya Android kwenda nyingine.
Kwenye Android 12 mtu ataweza kumtumia mtu mwingine password za WiFi anayotumia moja kwa moja kwenda simu nyingine na kuiwezesha simu hiyo kujiunga moja kwa moja kwenye WiFi husika bila mpokeaji kuingiza hizo password kikawaida.
Google wanajitahidi kufanya maboresho mengi kwenye Android ili kuifanya iwe rahisi kwa simu zijazo kutoka makampuni mbalimbali kuweza kupata masasisho kwa wakati na pia kufanya simu hizo kutotofautiana sana kiutendaji kazi. Jambo hili limekuwa changamoto kubwa kwa miaka iliyopita na lilikuwa linafanya baadhi kuchelewa au kukosa kabisa kupata masasisho ya matoleo mapya ya Android kutokana na uzembe wa makampuni yanayotengeneza simu hizo.
No Comment! Be the first one.