Tulio wengi duniani kote tunatumia WhatsApp ambayo mpaka hivi sasa ina zaidi ya watumiaji zaidi ya bilioni 2 lakini waswahili husema “Kizuri hakikosi kasoro”. Ndio, udhaifu wabainika kwenye WhatsApp.
Hivi itajisikiaje ghafla tuu unashangaa akaunti yako ya WhatsApp inasitishwa kwa muda bila ya wewe kufanya kitu chochote kinachoweza kufanya jambo hilo likatokea? Sasa fahamu hii leo kuwa timu ya watafiti wa masuala ya usalama kwenye vitu/vifaa vya kidijiti wamebaini udhaifu kwenye WhatsApp unaweza kusababisha akaunti yako ikafungiwa bila mwenye namba husika kufanya kosa lolote.
Ipo hivi wadukuzi wanaweza kujaribu kuingia kwenye kwenye akaunti yako ya WhatsApp iwapo watajua namba inayoitumia kwenye programu tumishi husika. Sote tunajua kuwa ili kuweza kuendelea na mchakato wa kufungua akaunti kwenye WhatsApp kuna zie namba zipatazo sita zinatumwa kwenda kwa mhusika (kwenye namba ya simu yenyewe).
Sasa kwakuwa wadukuzi hawatapata hizo namba za siri itawalazimu kujaribu jaribu na baada ya zoezi hilo kushindikana mchakato huo utasitishwa kwa muda wa saa 12 kwenye simu ya “Wadukuzi”. Kitakachofuata hapo ni ujanja kidogo tuu; wadukuzi watatengeneza barua pepe na kujifanya wao ndio wewe kisha kuwataarifu kuwa yeye mwenye namba hiyo ameibiwa na simu na hivyo wanaomba wasitishe matumizi ya WhatsApp kwenye akaunti husika. Hatimaye kitakachofuata ni kusitishwa kwa akaunti husika (yako).
Je, inawezekana kukwepa changamoto ya kusitishwa kwa akaunti yako ya WhatsApp?
Ieleweke kuwa mtumiaji hawezi kutumia akaunti yake kwa muda wa saa 12 (kipindi ambacho akaunti inakuwa imesitishwa) na baada ya muda huo kutimia wadukuzi wanaweza kurudi mtindo uleule na kusababisha kufungiwa tena kwa saa 12 nyingine sasa nini ufanye? Wakati wa kipindi hiki chote ambacho akaunti imesitishwa kwa muda mtumiaji anaweza kuwasiliana na watu wa kutoa msaada kwa njia ya barua pepe; tunashauriwa kutumia barua pepe wakati wa kusajili huduma ya “Two-step verification” ama kwa tafsiri isiyo rasmi hatua mbili za kufuata kabla ya kuingia kwenye akaunti.
Tunapotumia barua pepe kama njia ya kuongeza ulinzi wa kwenye akaunti zetu basi pale unakapowasiliana na WhatsApp kitengo cha huduma kwa wateja watakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuweza kutatua tatizo hilo.
Hata hivyo, haijabainika kama WhatsApp wanashughulikia ama tayari wameshashughulikia udhaifu huo uliogunduliwa na watafiti hivyo sote tunashauriwa kujiadhari na kujua nini cha kufanya tukikumbana na changamoto hiyo.
Vyanzo: Forbes, Gadgets 360
One Comment