Wakati habari za uzinduzi wa Samsung Galaxy Note 9 zilikuwa katika mitandao mbalimbali haikuelezwa kuwa siku ya utambulisho wa simu hiyo wangetambulisha saa janja yenye jina jipya, Galaxy Watch.
Ilikuwa ikitegemewa pengine Samsung wangezindua simu mbili kwa wakati mmoja lakini mambo yakawa tofauti na kuleta kwenye macho ya watu Galaxy Watch ambapo wahusika wameamua kutumia na jina tofauti, Samsung Gear (jina la zamani kwa saa janja za Samsung).
Galaxy Watch ina vitu vingi vizuri ambavyo kimsingi inafanya utofauti kati ya toleo la saa janja zilizopita na hii ya sasa zote zikiwa chini ya Samsung kwa sababu:
Aina. Hapa namaanisha saa hizi zipo za aina mbili; moja ina ukubwa wa 42mm na 46mm zote zikiwa zina kioo cha AMOLED urefu wa inchi 1.3. Mbali na hapo ili kuzuia michubuko kwenye kioo inalindwa na Corning Gorilla DX+.
Betri/kuchaji. Ile yenye ukubwa wa 46mm betri yake ina 472mAh na ndogo yake (42mm) ina 270mAh, zote mbili zinaelezwa kuduma na chaji kwa muda wa wiki nzima. Suala zima la kuchaji ndio inaweza kuwa kivutio kwani kimemeshi kina uwezo wa kuchaji Samsung Galaxy Note 9 na Galaxy Watch.
Mawasiliano. Saa zote mbili zina teknolojia ya LTE hivyo utaweza kupokea simu/ujumbe mfupi wa maneno na kuwweza kujibu hata kama upo mbali na simu yako. Pia zipo toleo jingine ambalo lenyewe linatumia Bluetooth.
RAM/Diski uhifadhi. Galaxy Watch ambazo zina teknolojia ya LTE zenyewe zina 1.5GB upande wa RAM, zile ambao zina Bluetooth RAM yake ni 768MB huku zote zikiwa na 4GB-Memori ya ndani.
Mikanda ya saa hiyo ipo katika rangi mbalimbali kama Nyeusi, Njano, Kawahia, Udhurungi, Maziwa na pamoja na mkanda wenye nembo ya Samsung iwapo hutavutia na rangi za mikanda hiyo.
Galaxy Watch inatumia Exynos 9110 dual-core yenye kasi ya 1.5GHz na programu endehi ni Tizen 4.
Kuanza kupatikana kwake ni mpaka Agosti 24 2018 kwa $330|Tsh. 759,000 (ukubwa wa 42mm) na $350|Tsh. 805,000 (ya ukubwa wa 46mm).
Vyanzo: Samsung, Tech Radar