Watanzania milioni 41 wanaomiliki simu za mezani na mkononi wametumia zaidi ya shilingi trilioni 6 kwa ajili ya kulipia muda wa maongezi ndani na nje ya nchi pamoja na kutuma ujumbe mfupi wa maneno (sms).
Kiasi hicho cha matumizi kilirekodiwa kwenye robo ya pili ya mwaka iliyoishia Juni ni kikubwa ikilinganishwa na shilingi 4.8 trilioni zilizotumika katika kipindi kama hicho mwaka jana.
Hata hivyo, kiwango hicho kinaweza kupungua kutokana na baadhi ya mitandao ya simu kuwa na vifurushi vya maongezi na sms ambavyo ni kwa ajili ya promosheni ya kuvutia wateja zaidi.
Kuongezeka kwa kiasi hicho ni kutokana na ongezeko la muda wa kupiga simu (dakika) na idadi ya ujumbe mfupi. Gharama nyingi isipokuwa kupiga simu nje ya nchi zilipungua katika vipindi hivyo vilivyofanyiwa uchambuzi.
Ripoti ya mawasiliano kwa robo ya pili ya mwaka iliyotolewa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), inaonyesha mpaka sasa jumla ya watu milioni 41.8 wanatumia simu tofauti na kipindi kama hiki mwaka uliopita ambapo watumiaji walikuwa milioni 40.3.