Apple wamezoeleka kutoa toleo jipya la iPhone kila mwaka lakini mara nyingi tarehe ya shughuli husika huwa haifahamiki waziwazi na hivyo basi watu kuishia kuwa na taarifa za kusadikika lakini sio kwa mwaka 2019!.
Kuna maneno ambayo watu wazima huwa wanapenda kuitumia inasema “Chunga sana kauli yako“. Maneno hayo nimeyatumia kwa lengo la kutaka kukueleza kisha ambacho kimemkuta rais wa kampuni inajishughulisha na utoaji wa huduma za mawasiliano, SoftBank huko Japan alijikuta akiweka wazi tarehe ya ujio wa toleo lijalo la iPhone bila kujua kuwa amevujisha siri 😆 😆 😆 .
Rais huyo wa SoftBank alijikuta akiweka wazi kuhusu ujio wa iPhone 11 (kama inavyofahamika kwenye tovuti nyingi) wakati akijibu swali kutoka kwa mwandishi wa habari kuhusu sheria mpya za mawasiliano huko Japan zitakapoanza kufanya kazi Oktoba Mosi itakayowataka kampuni za simu kutenganisha gharama za kupata huduma za intaneti na bei ya simu husika kwenye mikataba ya wateja ndipo alipojikuta akisema hana uhakika iwapo kampuni yake itaweza kusimamia uzinduzi wa iPhone ijayo ukizingatia itatoka siku 10 kabla ya sheria yenyewe kuanza kufanya kazi.
Kwa mujibu wa maneno hayo hapo juu inamaanisha kuwa toleo lijalo la iPhone litatoka siku kumi (10) kabla ya mwezi Septemba kuisha yaani Septemba 20 na ni wazi kuwa tarehe hiyo haipishani sana na tarehe ambazo toleo la nyuma lilitoka (Sept. 21 2018) kwa iPhone XS na XS Max huku iPhone XR ilikuja kutoka mwezi Oktoba kutokana na matatizo ya kiufundi ambayo yaliikumba simu janja husika.
Mara baada ya kugundua kuwa ametoboa siri kiongozi huyo wa ngazi ya juu kabisa ndani ya Softbank akajaribu kurekebisha kosa lake kwa kusema “Hakuna anayejua iPhone ijayo itatoka lini” lakni kama waswahili wanavyosema “Maji yakishamwagika hayazoleki“.
Vyanzo: GSMArena, Hype Beast