TikTok yaendelea kupingwa kuwepo nchini Marekani, hii ni baada ya Mkuu wa Shirika la Usimamizi wa Sekta ya Mawasiliano kuwaandikia na kuwataka wakurugenzi wa Google na Apple kuondoa app hiyo kutoka kwenye masoko ya apps ya Google Playstore na AppStore.
App ya TikTok kwa sasa ndio app inayokimbiza zaidi kwenye kundi la apps za mitandao ya kijamii. Imepakuliwa zaidi ya mara bilioni 3.5, huku ikiwa na wastani wa utumiwaji wa dakika 46 kwa siku kwa mtu. Vyanzo vinaonesha utumiwaji wa Instagram ni wastani wa dakika 28 – 29.
Afisa Brendan Carr wa Shirika la Usimamizi wa Sekta ya Mawasiliano – FCC (Federal Communications Commission), amesema app hiyo inabidi iondolewe kwa sababu za kiusalama wa data wa watumiaji wa nchi hiyo. Bwana Brendan amesema app hiyo ni kama vile imejifunika ngozi ya kondoo, ila ni silaha kubwa katika ulimwengu wa sasa wa usalama wa data.
TikTok bado wanasisitiza app yao ipo salama kabisa na kwamba hakuna linalofanyika la kutoa taarifa za watumiaji na data muhimu kwenda kwa serikali ya China.
Mgogoro huu umeanzia wapi?
Tokea kipindi cha serikali ya Rais Trump kulikuwa na juhudi za kuifungua kabisa app hii, kuchukua sera kama ile iliyochukuliwa dhidi ya Huawei. App ya TikTok imeanzishwa nchini China, ikimilikiwa na kampuni ya ByteDance yenye makao makuu Beijing, China. Kumekuwa na wasiwasi kutokana na sheria za nchini China, ni rahisi kwa kampuni/shirika kuzipa vyombo vya serikali uwezo wa kuchunguza data za watumiaji pale inapobidi kwa sababu za kiusalama na ulinzi.
Tiktok waliponea kufungiwa kipindi hicho baada ya kukubali kutenganisha eneo ambalo data za watumiaji zinahifadhiwa. Waliingia makubaliano na kampuni ya Oracle, kuweza kuhifadhi data za watumiaji wa Marekani na mataifa mengine ya magharibi kwenye huduma za uhifadhi data za Oracle zilizopo nchini Marekani.
Kwa nini wanapingwa tena?
Hivi karibuni wafanyakazi wa TikTok wa nchini Marekani walivujisha siri ya kwamba bado wafanyakazi wa TikTok waliopo nchini China wanapewa uwezo wa kuangalia data za watumiaji wa Marekani. Na ata uongozi wa TikTok wa Marekani ulipobanwa kuhusu jambo hili majibu yameonesha kuna uwezekano mkubwa jambo ni la kweli.
Bwana Carr wa FCC amewapa Google na Apple hadi Julai 8 kutoa majibu kuhusu uamuzi wa kuiondoa app hiyo kutoka kwenye masoko yao ya Apps.
Ingawa FCC haina mamlaka juu ya masuala ya mitandao ya kijamii ya kutumika, ila wana nguvu kama huduma husika inaweza kutumiwa kudukua au kuharibu mifumo ya kimawasiliano.
Vyanzo: CNBC na vyombo mbalimbali
No Comment! Be the first one.