Mamlaka ya mawasiliano nchini (TCRA) imepunguza viwango vya gharama za mawasiliano ya simu kutoka shilingi 26.96 kwa dakika iliyokuwa ikitozwa mwaka huu hadi shilingi 15.60 itakayoanza rasmi kutumiwa mwakani.
Viwango hivyo vipya vitaanza kutumika Januari Mosi mwaka 2018. Mkurugenzi mkuu wa mamlaka hiyo, Mhandisi James Kilaba amesema gharama hizo zitaendelea kupungua kila mwaka hadi zifikie shilingi mbili ifikapo mwaka 2022. Hatua itakayochochea idadi ya watumiaji wa mawasiliano na hivyo kuongeza pato la watoa huduma na taifa kwa ujumla.
Wakati umuhimu wa huduma za mawasiliano ukizidi kuongezeka, gharama za mwingiliano wa mitandao ya simu ambazo kwa sasa ni shilingi 26.96 kwa dakika zinaonekana kuwa ni kikwazo kwa watumiaji wengi ambao wameitaka TCRA kuzifuatilia kampuni za simu zenye tabia ya kupandisha gharama za vifurushi na aina nyinginezo kiholela na hivyo kuwaibia wateja.