App maarufu ya kuchati duniani, WhatsApp, inakuja na uwezo mpya utakaowawezesha watumiaji wake kutazama video za YouTube moja kwa moja katika WhatsApp bila uhitaji wa kwenda popote pale mtu akishare linki ya video hizo.
Kwa muda mrefu hali imekuwa ni tofauti kidogo, kama mtu atatuma linki ya video kutoka mtandao wa YouTube kwenye app ya WhatsApp basi mpokeaji ilimbidi abofye na kisha apelekwe kwenye kivinjari (browser) au app ya YouTube ili aweze kutazama video hiyo.
Katika masasisho yanayoletwa na WhatsApp basi mpokeaji ataweza kutazama video hiyo moja kwa moja ndani ya app hiyo. Pia wakati video hiyo ikiendelea kutazamwa basi mtumiaji ataweza kuendelea kuangalia mazungumzo mengine kwenye eneo lake la kuchat huku video hiyo ikiendelea kucheza.
Pia maboresho katika eneo la kurekodi ujumbe wa sauti.
Zamani ili kuweza kurekodi ujumbe basi ilikubidi ubofye na kuendelea kushikilia kitufe cha kurekodi mwanzo hadi mwisho wa ujumbe unaorekodi. Mabadiliko mapya ni kwamba hakuna tena uhitaji wa wewe kuendelea kushikilia kitufe hicho muda wote.
Utaweza kubofya mara moja na kuachia kuruhusu kurekodi ujumbe wako, utakapomaliza kuongea basi utabofya kutuma ujumbe wako.
Mambo haya mapya yameanza kuonekana kwa baadhi ya watumiaji wa WhatsApp kwenye simu za iPhone (iOS) na inategemewa toleo hilo litaanza kusambaa pia kwa watumiaji wengine wote ndani ya kipindi cha hizi siku chache.