Muendelezo wa maandamano nchini Marekani dhidi ya matukio ya kibaguzi yamelazimisha makampuni ya Sony na Google kuhairisha shughuli zao za utambulisho wa PlayStation 5 kwa Sony, na toleo lijalo la Android kwa Google.
Makampuni hayo yamefanya hivyo ili kutoonekana kama yanadharau umuhimu wa maandamano yanayoendelea katika majiji mbalimbali ya nchini Marekani.
Google na toleo lijalo la Android 11
Juni 3 hii ilikuwa ni siku ya Google kutambulisha rasmi toleo la Android 11, katika kiwango cha BETA. Lengo likiwa watu na hasa hasa watengenezaji apps waweze kuelewa kwa undani kuhusu mapya yanayokuja katika toleo hili la Android.
Toleo hili la Android linakuja na uwezo mzuri wa kufanya kazi na teknolojia mpya kama za 5G, uchezaji wa video za ubora wa 4K na pia uwezo wa kuhimili uchezaji magemu wa ubora wa juu.
Sony na PlayStation 5
Toleo la Sony PlayStation 5 linasubiriwa kwa hamu kwa kuwa Sony wamefanya mabadiliko makubwa kwenye muonekano wake na pia kuna maboresho yanayovutia ukilinganisha na toleo la PS 4.
Kiuwezo/ufanisi PlayStation 5 inakuja ikiwa inatumia prosesa ya AMD Zen 2 (8 Cores, 3.5GHz), RAM ya GB 16, diski ya uhifadhi itakuwa ya mfumo wa SSD, na mfumo wa CD utakuwa unakubali hadi CD za kiwango cha 4K. Magemu yaliyotengenezwa kwa ajili ya PS 4 yataweza kutumika bila matatizo.
Je simu yako inatumia toleo gani la Android? Je unadhani kwako huwa ni muhimu kutumia toleo la kisasa zaidi la Android?
Endelea kutembelea TeknoKona.