Fahamu kuhusu Slide Safe. Huko nchini Nigeria/Naijeria vijana kadhaa waungana na kuanzisha huduma ya uuzaji wa vifaa vya kujipima binafsi maambukizi ya VVU – yanayosababisha UKIMWI.
Huduma hiyo waliyoipa jina la Slide Safe inawasaidia watu kuepukana na ugumu wa kuingia kwenye maduka ya dawa na vituo vya upimaji ukimwi. Nigeria kama mataifa mengine mengi ya Afrika bado vijana wengi wanaepuka kwenda kupima viambukizi vya VVU mara kwa mara.
Kiboksi kimoja kinaweza kuwa na gharama kati ya dola 5 hadi 20 (Tsh 10,000 – 45,000/=) kulingana na bidhaa iliyonunuliwa. Bidhaa zinazopatikana ni vipimo vidogo vya kujipima maambukizi ya VVU, kondomu na vilainishi.
Wengine wanashindwa kwa kuogopa kuchukuliwa tofauti na jamii inayowazunguka. Kupitia huduma hii iliyopewa jina la Slide Safe lengo kubwa ni kuhakikisha mwenye nia ya kujipima yeye au kupima yeye na mwenzi wake wanaletea vifaa hivyo kwa usiri bila mtu kujua nini hasa wameletewa kwenye viboksi wanavyoletewa.
Manunuzi ni kupitia njia ya mtandao, kisha watu wa Slide Safe watakuwekea vipimio hivyo kwenye boksi lisiloonesha alama yeyote ya kwamba ni mzigo wa kipimo cha HIV. Pia kuna njia ya simu, unaweza kuandaa jinsi ya kupata mzigo kwa kutumia SMS na kulipa pale utakapoletwa.
Huduma hiyo imeanzishwa na Bi Florida Uzoaru mwezi wa kwanza mwaka huu akiwa chuo kikuu cha Lagos. Tayari anatafuta wawekezaji zaidi ili kuweza kupata mtaji mkubwa zaidi ili kuweza kuikuza huduma hiyo zaidi.
Nigeria ni moja ya nchini yenye kiwango kikubwa sana cha maambukizi ya VVU, ina idadi ya watu milioni 3.2 wanaoishi na VVU. Nigeria, Uganda pamoja na Afrika Kusini kwa pamoja huwa zinachangia nusu ya maambukizi yote mapya ya VVU duniani kila mwaka.
Je unalionaje wazo hili? Je unadhani huduma kama hii inaweza saidia vijana wa Tanzania pia kufanya maamuzi ya kujua afya zao na kununua na kutumia kinga?
Chanzo: QZ.COM, Slide Safe.