Simu zenye 5G kuja mwaka 2019. Upo hapo?
Wakati bado kwa nchini mfumo wa 4G ndio umezidi kuimarika maeneo mbalimbali kupitia mitandao kadhaa ya simu tayari teknolojia ya 5G inaonekana ipo tayari kuingia sokoni.
Kampuni nguli katika utengenezaji wa vipuli mbalimbali muhimu vinavyotumika kwenye simu janja nyingi duniani, ya Qualcomm, imesema tayari inashirikiana na makampuni na mitandao kadhaa ya simu duniani kote ili kuleta simu zenye teknolojia ya 5G ndani ya mwaka 2019.
Qualcomm ni kampuni inayotengeneza vifaa vidogo mbalimbali vya teknolojia ya mawasiliano ambavyo hutumika ndani ya simu na pia kwenye mitambo mikubwa ya mitandao ya simu.
Kampuni hiyo imesema modemu ya mawasiliano itakayotumiwa kwenye simu na kuwezesha teknolojia ya mawasiliano ya 5G tayari ipo kutumika na ushirikiano ni mkubwa tuu na makampuni kadhaa ya simu, ila cha ajabu si Apple, wala Samsung, wala Huawei…..wanashirikiana na Qualcomm.
Qualcomm Snapdragon X50 5G NR Modem, modemu ya mawasiliano iliyotengenezwa na Qualcomm, simu zenye modem hii zitakuwa na uwezo wa mawasiliano ya 5G.
Qualcomm wamesema kuna makampuni 18 makubwa yanayoshirikiana nayo, hii ni pamoja na Nokia/HMD, Sony, Xiaomi, Oppo, Vivo, HTC, LG, Asus, ZTE, Sharp, pamoja na Fujitsu.
Kulingana na mtandao wa TheVerge, kampuni ya Huawei inaeleweka haitumii modemu za Qualcomm katika simu zake, ila Apple na Samsung wote wanatumia modemu hizo. Samsung amekuwa akitoa simu zinazotumia modemu walizotengeneza wenyewe, Exynos, na pia kuna matoleo yanayotumia modemu za Qualcomm.
Baadhi ya mitandao ya simu ambayo imeingia katika ushirikiano na Qualcomm katika kuwezesha huduma ya mawasiliano ya 5G katika majaribio hapo mwakani ni AT&T, British Telecom, China Mobile, Deutsche Telekom, Orange, SK Telecom, Sprint, Telstra, Verizon, pamoja na Vodafone.