Wengi walitegemea Samsung wangeonesha tuu simu hii na kusema itatoka mwishoni mwa mwaka au hata mwakani, ila Samsung wametambulisha na kusema itaanza kupatikana ndani ya miezi miwili kuanzia sasa – yaani Samsung Galaxy Fold itapatikana Aprili.
Samsung wamekuwa na lengo la kuleta simu hii kwa muda sasa na miezi michache iliyopita Xiaomi walionesha ya kwao na hivyo ukawepo uwezekano wa wao (Xiaomi) kuwapiku Samsung kwa kuwa wa kwanza kuleta simu ya namna hii sokoni ila kumbe Samsung wapo mbele zaidi – simu ipo tayari kuingia sokoni.
Je, Samsung Galaxy Fold ni simu ya namna gani?
Kama jina lake lilivyo, ‘Fold’ ni kimombo cha kukunja/mkunjo, Galaxy Fold ndio jina waliloipa simu yao yenye uwezo wa kutumika kama simu na kisha pia kuweza kufunguliwa na kupata uso mpana zaidi na kuwa tabiti.
Simu ya Galaxy Fold ikiwa imekunjwa ina kioo/display kidogo mbele ambacho unaweza kutumia kama simu ya kawaida wakati Galaxy Fold ikiwa katika umbo dogo – la inchi 4.6.
Pale utakapotaka kuitumia kama tabiti basi utaifungua na ndani ya sekunde moja programu tumishi yoyote uliyokuwa unaitumia wakati huo itajifungua kwa upana katika display/kioo cha ndani cha inchi 7.3 (sentimeta 18.5).
Ukubwa huu unaifanya katika umbo la tabiti iwe na uwezo wa kufungua app tatu kwa wakati mmoja mbele ya mtumiaji kwenye display hii kubwa.
Kiungo chake kinachounganisha pande mbili Samsung wamesema wametumia teknolojia ya kisasa sana kuhakikisha kitadumu mara maelfu ya ufunguaji na ufungaji. Pande zote mbili zinahifadhi betri kuhakikisha kifaa hiki kinadumu na chaji muda mrefu – mAh 4380.
Galaxy Fold ina maeneo matatu yenye kamera – Nyuma kuna kamera tatu, ndani kwa ajili ya selfi kipindi unaitumia kama tabiti kuna kamera mbili, wakati unaitumia kama simu kuna kamera moja ya selfi.
Sifa nyiingine;
- Inakuja na RAM ya GB 12,
- prosesa ambayo Samsung hakuitaja – inaaminika itakuwa ni ya kwao na si Snapdragon.
- Diski ujazo ni wa GB 512.
- Inakuja na uwezo wa 4G na toleo la 5G lipo njiani.
Katika bidhaa ambazo Samsung wametambulisha hivi karibuni hii ndio bidhaa isiyo na uhakika sana wa hali ya soko. Ukiangalia bei yake ni kubwa sana na hili linaweza kuwafanya watu kuona ni rahisi zaidi kuwa na kununua tabiti na simu kama vitu tofauti.