Utafiti unaonesha takribani simu janja milioni 900 zinazotumia Android na zikiwa na teknolojia ya chip kutoka kampuni ya Qualcomm zipo hatarini dhidi ya udukuzi.
Watafiti kutoka kundi la utafiti wa kiusalama la CheckPoint, wamegundua makosa ya kiusalama yanayoweza wezesha wadukuzi kudukua kwa urahisi simu nyingi sana zinazotumia Android na huku zikiwa na chip za Qualcomm.
Kivipi?
Inasemekana kama mtu akipakua app isiyo salama baada ya kudanganywa na wadukuzi – wadukuzi hao watapata nguvu ya kupata data mbalimbali kuhusiana na simu husika.
Aina ya simu zilizoathirika
- BlackBerry Priv na Dtek50
- Blackphone 1 na Blackphone 2
- Google Nexus 5X, Nexus 6 na Nexus 6P
- HTC One, HTC M9 na HTC 10
- LG G4, LG G5, na LG V10
- New Moto X ya Motorola
- OnePlus One, OnePlus 2 na OnePlus 3
- Samsung Galaxy S7 na Samsung S7 Edge
- Sony Xperia Z Ultra
Hakuna ushahidi kuwa tayari simu hizo zimeathirika ila ukweli ni kwamba mtu yeyote mwenye ufundi na nguvu kubwa katika udukuzi inasemekana anaweza akafanikiwa kuingilia simu hizo. Chip za kampuni ya Qualcomm zinazodaiwa kuja na matatizo katika ‘drivers’ zake za Android inasemekana zipo katika takribani simu milioni 900. Hilo linamaanisha kuwa simu milioni 900 zipo katika hatari kubwa ya kudhibitiwa na wadukuzi.

Upungufu unamwezesha mtu wa tatu kumpokonya mmiliki wa simu udhibiti kwani anaweza hata akabadilisha nywila (password) bila yako wewe kujua. Njia moja ya kuimarisha usalama wa simu ni kupata apps kutoka kwa soko maalum la Google Play.
Ila inasemekana tayari kuna simu ambazo zishapata masasisho (updates) yanayoongeza usalama na hivyo kuweka salama simu hizo. Na pia Google na Qualcomm wamesema tayari kuna masasisho mengine yanakuja kwa ajili ya simu nyingi zaidi.
Vyanzo: The Times of India, BBC