Ikulu ya Marekani, White House inafikiria kupiga marufuku wafanyakazi wake kutumia simu janja binafsi wakati wa kazi kutokana na wasiwasi wa kudukuliwa kwa mawasiliano katika Ikulu hiyo.
Taarifa zinasema kumekuwa na simu janja nyingi binafsi za wafanyakazi wa Ikulu hiyo ambazo zinaonekana kuungwa kwenye mitandao kupitia Wi-fi ya West Wing iliyopo ndani ya White House. Mkuu wa White House John Kelly ambaye simu yake iliathiriwa na wadukuzi mapema mwaka huu binafsi yupo mstari wa mbele kupitishwa kwa marufuku hiyo.
Simu janja zilizotolewa na White House kwa wafanyakazi wake haziwezi kutuma ujumbe wa maandishi hivyo kuzuia malalamiko ya wafanyakazi hao kushindwa kuwasiliana na na familia zao pindi wanapohitaji kufanya hivyo kwa njia ya ujumbe mfupi.
Aidha, kompyuta zinazotumiwa na wafanyakazi wa ikulu ya Marekani zimezuiwa uwezo wa kutuma ujumbe kupitia Gmail, Google Hangout na baadhi ya tovuti fulani kushindwa kufunguka hivyo kuwalazimu kutumia simu zao binafsi.
Wakati wa ziara ya rais Trump nchini China wafanyakazi wa ikulu walioambatana na Rais walizuiwa kutumia simu zao za kawaida kwa wasiwasi wa kudukuliwa mawasiliano yao wakiwa huko.
Hatua rasmi ya upigaji marufuku bado kwa kuwa kumekuwa na mjadala wa pande mbili za wale wanaotaka na wasiotaka marufuku hiyo. Rais Donald Trump amelalamika mara kwa mara juu ya uvujaji wa taarifa za Ikulu kwa vyombo vya habari tangu kuchukua ofisi.