Simu janja kutoka Xiaomi zimekuwa zikishika kasi kwa maana ya kwamba zinanunuliwa kwa wingi na hivyo kuleta ushindani wa aina yake kwa makampuni kama Apple, Samsung. Masasisho kwenye vitu vya kiteknolojia ni muhimu sana ingawa mambo ni tofauti kidogo.
Hata kama hauna simu janja yoyote kutoka Xiaomi lakini kama ni mfuatiliaji wa makala zetu mbalimbali juu ya uchambuzi wa simu janja mbalimbali za Xiaomi utakuwa unajua kuwa simu hizo moja ya sifa zake ni kuja na MIUI (ipo kwenye simu janja/tabiti za Xiaomi).
Simu janja 6 ambazo hazitopata tena masasisho ni Mi 2/2S, Mi 4i, Redmi Note 4G, Redmi 2, Redmi 2 Prime, na Mi Note ambapo masasisho ya mwisho kwa simu janja tajwa itakuwa ni MIUI Beta ROM 7.11.16. Sababu ya kuachana na kuendelea kutoa masasisho kwenye simu janja hizo umwzingatia mwaka uliotolewa simu husika, watu ambao bado wanatumia simu hizo, uwezo wa simu janja.
Xiaomi imetoa MIUI 9 kama toleo la majaribio lakini ambalo halitahusisha simu janja ambazo zimeorodheshwa kuacha kupokea masasisho yoyote kutoka Xiaomi.
Kuna wakati inafikia lazima tukubaliane na mabadiliko kutokana na sababu mbalimbali hasa katika ulimwengu wa teknolojia ambao kila siku unakuja na kitu kipya. Masasisho ya mwisho kwenye simu hizo yataanza kupatikana kuanzia mwezi Desemba mpaka Januari 2018.
Vyanzo: Gadgets 360, India Express