Huawei watambulisha rasmi simu yao ya Huawei Mate 9 inayoonekana kuwa na uwezokano mkubwa kufanikiwa zaidi kutokana na majanga yaliyoikuta simu ya Samsung Galaxy Note 7.
Huawei Mate 9 inakuja katika matoleo mawili, moja ni la bei ya dola 775 za Marekani (takribani Tsh 1,700,000/=) na pia kuna toleo spesheli lililobuniwa na kampuni ya ubunifu ya Porsche – toleo la Huawei Mate 9 Porsche Design itauzwa kwa dola 1,500 za Marekani (zaidi ya Tsh 3,000,000/=).
Simu ya Huawei Mate 9 inalenga wateja wenye uwezo kutumia pesa nyingi kiasi kwa ajili ya kununua simu. Huawei Mate 9 inalenga kushindana moja kwa moja na simu kama vile iPhone 7 Plus na Google Pixels XL.
Sifa kwa ufupi
Mate 9 inakuja na display ya inchi 5.9. Ndani yake ina prosesa ambayo wenyewe wamesema ni moja ya prosesa ya kiwango cha juu kwa sasa sokoni – Octa-core Kirini 960. Nguvu inaongezwa kwa uwepo wa RAM ya GB 4 pamoja na diski uhifadhi (storage) GB 64.
Inakuja na uwezo wa laini mbili ila eneo moja la laini linaweza tumika kama sehemu ya kuwekea memori kadi(Micro SD Card).
Inakuja na betri ya mAh 4,000 ambayo Huawei wanasema inaweza dumu hadi masaa 48 kwa utumiaji wa kawaida. Mfumo wa kuchaji umekuja na teknolojia ya kuchaji kwa haraka ‘fast charging’ na hivyo utaweza kuchaji kutoka 0 hadi asilimia 58 ndani ya dakika 30. Hii ni haraka zaidi kwa takribani mara mbili ukilinganisha na uwezo wa simu ya iPhone 7.
Kwenye kamera je?
Huawei Mate 9 inakuja na kamera mbili katika eneo moja nyuma. Kamera hizi zimetengenezwa na kampuni mashuhuri katika masuala ya kamera ya Leica.
Kamera ya juu inakuja na sensor ya MP 12 wakati chini yake kuna ya Megapixel 20. Kamera hizo zinazotumika kwa wakati mmoja wakati wa upigaji picha au kurekodi video zinasaidia kuhakikisha ubora wa juu.
Chini tuu ya kamera hiyo ya nyuma kuna eneo la fingerprint sensor.
Kuna nini kwenye Mate 9 Porsche Design?
Toleo la Mate 9 Porsche Design linalenga watu wachache tuu.. Watu wenye uwezo wa kutoa pesa zaidi kwa ajili ya maboresho kiasi ila kitu kikuu ikiwa ni sifa ya kuwa imebuniwa na kampuni nguli ya ubunifu ya Porsche. Sifa zingine zote ni sawa na toleo la Mate 9 la kawaida na tofauti zipo kadhaa;
- Nayo inakuja na ‘body/housing’ iliyotengenezwa kwa kutumia aluminum. Kwa toleo hili muonekano wote umefanyiwa kazi ya ubunifu kwa kiasi kikubwa na kampuni ya Porsche.
- Ukubwa wa display wa inchi 5.5 chenye uwezo wa kuonesha picha za ubora wa kiwango cha 2K (Resolution).
- Pia display yake imesogea hadi pembeni mwa simu hiyo – kufanana na simu za matoleo ya Samsung Edge.
- Prosesa ni kama ya toleo la kawaida la Mate 9 ila hii inakuja na RAM ya GB 6 na uhifadhi (storage) wa GB 256 ndani yake.
Kutakuwa na jumla ya simu 20,000 tuu za Huawei Mate 9 Porsche Design. Kwa bei ya zaidi ya milioni 3 za Kitanzania haishangazi kuona uamuzi wa kampuni hiyo kutengeneza simu chache tuu.
Programu endeshaji: Android 7
Simu zote zinakuja na toleo la Huawei EMUI 5.0 ambalo limetengenezwa juu ya toleo la Android 7. Ili kujiweka kiushindani zaidi Huawei wamefanya uamuzi wa kupunguza idadi ya apps zinazokuja moja kwa moja na simu hiyo.
Inasemekana simu nyingi huanza kupunguza kasi ya utendaji (performance) baada ya miezi 6 ya kutumika – kuepuka hali hii kwa Mate 9 Huawei wametengeneza teknolojia ya kusaidia simu kujisafisha na kuhakikisha utendaji unakuwa bado wa hali ya juu kwa zaidi ya miezi 18 ya kutumika – hii ni kwa madai yao!
Upatikanaji: Simu hizi zitaanza kupatikana muda wowote kuanzia sasa hadi mwezi wa kumi na mbili.
Mtazamo wetu
Huawei wamefanikiwa kuwa kampuni ya simu kutoka China iliyoweza fanikiwa sana hadi katika masoko ya simu ya Ulaya na Marekani. Kuna uwezekano mkubwa toleo hili likaweza kufanya vizuri sokoni, hasa hasa wakiwa katika eneo zuri la kunufaika na janga lililoikuta Samsung na toleo la Samsung Note 7.
One Comment
Comments are closed.