Serikali ya Uganda imetangaza kwamba sheria mpya ya tozo ya kodi kwenye mitandao ya kijamii itaangaliwa upya kufuatia maandamano yaliyofanyika nchini humo.
Hata hivyo, hakuna uhakika kuwa kodi hiyo itaondolewa kabisa au huenda ikachukua wiki kadhaa kabla ya kuidhinishwa mabadiliko yoyote yale.
Serikali ya Uganda ilipitisha sheria ambayo ilianza kutumika Julai Mosi ambayo inatoza kodi ya shilingi za Uganda 200 kila siku kwa anayetaka kutumia mitandao ya kijamii.
Tamko la serikali limekuja baada ya siku ya Jumatano kufanyika maandamano makubwa ya wananchi kupinga kuwepo kwa kodi hiyo inayomuumiza mwananchi.
Maandamano hayo yaliongozwa na mbunge na mwanamuziki nchini Uganda Robert Kyagulany, maarufu kama Bobi Wine ambapo polisi walijaribu kumkamata lakini alifanikiwa kutoroka.
Polisi walilazimika kurusha mabomu ya gesi ya kutoa machozi na kufyatua risasi hewani ili kutawanya kundi la waandamanaji wanaopinga kodi iliyoidhinishwa ya kutumia mitandao ya kijamii.