Samsung kampuni inayoongoza kwenye mauzo ya deki za diski za Blu-ray duniani imesema ina mpango wa kuachana na biashara ya utengenezaji wa diski hizo. Huduma za kuangalia mtandaoni – streaming, inaonekana kuchangia moja kwa moja uamuzi huu wa Samsung.
“Samsung haitaingiza toleo lolote jipya sokoni”, alisema msemaji wa Samsung nchini Marekani, akiongelea suala hilo kwa soko la nchini humo
Teknolojia ya diski za Blu-ray ilileta uwezo mkubwa wa watumiaji wa kawaida majumbani kuweza kuangalia filamu katika ubora wa HD ya hali ya juu – ikiwa ni kwenye mifumo ya HD ya 1080p au 4K. Diski za Blu-ray zilikuja kama mbadala wa teknolojia ya diski za DVD ambazo hazikuwa na uwezo wa kuhifadhi data za ukubwa zaidi ili kufanikisha uhifadhi wa filamu zenye ubora wa juu bila ulazima wa kutumia diski nyingi.
Historia yake kwa ufupi
Teknolojia ya diski za Blu-ray ilitengenezwa na Sony kwa ushirikiano na Panasonic, Philips na TDK kuelekea mwaka 2000. Na baada ya muda mrefu wa kuweka sheria za viwango vya ubora na usalama wa data, pamoja na kuwezesha makampuni ya filamu kuanza kutumia teknolojia hii katika utengenzaji wa filamu zao….mwaka 2006 ndio deki ya kwanza yenye uwezo wa kucheza diski za Blu-ray iliingizwa sokoni na Samsung.
- Filamu maarufu za kwanza kuingia sokoni zikiwa na matoleo ya diski za Blu-ray ni pamoja na The Terminator, 50 First Dates, Underworld: Evolution pamoja na xXx.
- Kwa mara ya kwanza, Januari 2007 ndio mauzo ya filamu katika diski za Blu-ray zilipiku mauzo ya diski ya mfumo wa DVD. Hii ni baada ya watumiaji wengi wa majumbani kuanza kuwa na umiliki wa deki zenye uwezo wa kucheza mfumo huo wa diski – wakihitaji kuona muvi kwenye kiwango kikubwa zaidi cha ubora.
- Diski moja ya Blu-ray inauwezo wa kubeba kati ya GB 7 hadi GB 100 ya data kulingana na aina ya diski.
- Uamuzi wa Samsung unaonekana kuchangiwa zaidi na ukuaji mkubwa wa huduma za kustream mtandaoni kama vile Netflix, Hulu, Amazon na nyinginezo. Kupitia huduma hizi wengi wanaweza kutazama filamu katika mfumo wa HD wa hadi 4K bila uhitaji wa kununua diski zozote. Hivyo wameshaona mauzo ya deki zao hayatakuwa mazuri mbeleni.
Data za kimauzo zinaonesha Samsung bado yupo juu kwenye soko akiwa na asilimia 37 ya soko la deki za 4K Blu-ray, huku akifuatiwa na Sony – asilimia 31, LG – asilimia 13 na wengine wakichukua asilimia zilizobaki.
Kwenye masoko ya nchi kama zetu diski hizi pamoja na deki zake hazikupata umaarufu sana, sababu kubwa inaweza ikawa ni bei. Wakati kwa sasa bei ya deki ya 4K Samsung inacheza kuanzia kati ya Tsh. 500,000 hadi Tsh. 1,000,000 na filamu za 4K pia ni bei ya juu kuliko za DVD za kawaida. Sababu nyingine ni kwamba haina maana kuwa na deki ya 4K kama runinga yako haina uwezo wa kucheza filamu kwenye ubora huo.