Kwa muda mrefu tumekuwa tukinufaika sana na uwepo wa chaguo la kuweka memori kadi (SD Card) katika simu janja zetu lakini sasa kuwa tayari kuona uwezo huo ukiondoka kwenye baadhi ya simu janja za hadhi/kiwango cha juu zaidi.
Tumezoea hali hii kuiona kwa simu na tableti kutoka kampuni ya Apple ambao kwa miaka mingi kila wanapokuwa na toleo la simu au tableti wamekuwa wakitoa ya aina tatu, tofauti kuu ikiwa ni ujazo na kwa kwenye ujazo zaidi kunakuwa na bei ya juu zaidi. Na sasa makampuni mengi zaidi yanaanza kufanya hivyo pia.
Kwa mfano katika simu za iPhone 6 na ata Samsung Galaxy S6 kuna matoleo ya ujazo tofauti, GB 32, GB 64 na GB 128, simu hizi zisizokuwa na eneo la kuweka memori kadi zinakuwa zinatofautiana kwa gharama kubwa sana kutokana na utofauti wa ujazo wa diski.

Makampuni mengi ya utengezaji simu yameanza kuchagua kufanya hivyo pia, kuondoa eneo la kuweka memori kadi na kuamua kukuletea toleo la simu moja katika bei tatu, tofauti kuu ikiwa ni ujazo wa diski yake uhifadhi wa ndani (Storage). Kwa mara ya kwanza uamuzi huu umeonekana kwa ukubwa baada ya kampuni ya Samsung kupitia toleo lake maarufu la simu za aina ya Galaxy S, simu zake za Galaxy S6 na S6 Plus haziji na uwezo wa kuwekewa memori kadi kama ilivyokuwa kwa matoleo mengine kabla yake.
Jiandae, kama unataka simu janja ya kuvutia zaidi na iliyobora, basi utalipa zaidi pia kama unataka nafasi kubwa ya ujazo wa diski uhifadhi (storage)
Hivi karibuni kupitia mtandao wa habari za kiteknolojia wa Engadget katika mahojiano yake na mmoja wa afisa wa kampuni ya simu inayokuja kwa kasi zaidi, Xiaomi, makamu rais wa kampuni hiyo Bwana Hugo Barra ametoa sababu ya maamuzi hayo.
“Kwa ajili ya vifaa vyenye utendaji mkubwa wa kazi, tunapinga uwepo wa eneo la kuweka memori kadi” – Barra, Kampuni ya Xiaomi
“Memori kadi zinasababisha apps na simu kwa ujumla kutofanya kazi vizuri”
Bwana Barra amesema uwepo wa memori kadi feki au zenye ubora wa chini kama sababu kubwa ya kupinga uwepo wa sehemu ya memori kadi katika simu janja za kiwango cha juu. Amesema watumiaji huwa wanalalamika kuhusu simu kuwa nzito kiutendaji (slow), na upotevu wa data na matatizo mengine mengi huku wakifikiri ni tatizo la simu zao ila mara nyingi wanakuta huwa inasababishwa na utumiaji wa memori kadi zenye kiwango kibovu. Amedai pia uwepo wa memori kadi nyingi zinazotengenezwa katika viwanda bubu na kisha kutumia nembo za Kingston na SanDisk, na hivyo watumiaji wengi wanakuwa wakiamini ya kwamba wana memori kadi ‘original’ kutoka makampuni husika kumbe inakuwa sio hivyo.
Je, ni kweli?
Si kweli, kama umemiliki simu janja mbalimbali katika kipindi kirefu na kufanikiwa kutumia memori kadi utatambua hilo sio tatizo. Ata memori kadi za bei rahisi mara nyingi haziwezi kuathiri utendaji kazi wa simu yako au apps yako. Kiukweli uamuzi wa makampuni haya kuamua kuondoa eneo la memori kadi ni UAMUZI WA KIMAPATO ZAIDI! – KIBIASHARA NA SI SUALA LA UTENDAJI! Kama suala lingekuwa hilo wangeendelea kuuza simu zenye uwezo huo wakiambatanisha na memori kadi na watu wachague wenyewe kama hawaziitaji. Na cha ajabu zaidi ni kwamba kampuni kama Samsung tayari inajikita zaidi katika utengenezaji wa memori kadi.
Ukichunguza kwa haraka katika simu au tableti za Apple na ata kwa sasa kwa simu hizi za Galaxy kutoka Samsung utagundua ya kwamba tofauti hii ya ujazo katika toleo la simu flani linahusisha pia tofauti kubwa ya bei na mara nyingi ni zaidi ya ata laki 2 na kuendelea kwa tofauti ya GB 16 – 32 katika ujazo wa diski uhifadhi wa ndani. Bei hii ni kubwa sana ukilinganisha na bei za memori kadi. Unaweza ukapata memori kadi yenye ujazo wa ata GB 32 kwa gharama ndogo zaidi kulinganisha na tofauti ya bei ya simu ya toleo la GB 16/32 na 64.

Hivyo kuanzia sasa tambua ya kwamba simu janja za kiwango cha juu kwa ubora zitakazokuwa zinakuja nyingi sana hazitakupa uwezo wa kutumia memori kadi tena, hivyo kama utakuwa unataka nafasi kubwa zaidi basi jitayarishe kutumia pesa zaidi. Njia nyingine unayoweza kutumia ni kutumia teknolojia ya ‘Cloud’, uhifahamu? Bofya hapa -Umesikia kuhusu GB zako za Bure?
Endelea kutembelea mtandao wako namba moja kwa habari na maujanja ya kiteknolojia Tanzania!
[Kama ulikuwa haufahamu kampuni ya Xiaomi soma hapa -Xiaomi yauza simu Milioni 2 ktk Masaa 12, Rekodi ya Dunia ya Guinness Yawekwa]
No Comment! Be the first one.