Serikali ya Rwanda imepiga marufuku matumizi ya simu za mkononi kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari kwa kile kilichodaiwa ni kupambana na kulinda maadili yao.
Wizara ya jinsia na kukuza familia ilitoa taarifa hiyo siku ya Alhamisi katika mkutano na waandishi wa habari kupitia Waziri wake, Bi. Esparance Nyirasafari ambapo uamuzi huo umepitishwa na baraza la mawaziri katika kampeni ya kupunguza uhalifu wa utekaji watu nyara kupitia simu.
Simu za mkononi zinaweza kuwa rahisi kwa wahalifu kuwafikia wanafunzi akitoa mfano wa wafanyabiashara wa kuteka watu ambao wamekuwa wakiwafatilia watu kwa kutumia simu za mkononi na mara nyingi waathirika wamekuwa ni wasichana wadogo na wavulana~Bi. Esparance Nyirasafari.
Uamuzi huo unawataka wazazi kuwazuia watoto wao kwenda na simu shuleni kwa kuziacha nyumbani. Na endapo mwanafunzi atakutwa na simu shuleni atarudishwa nyumbani kumwita mzazi wake na kupewa onyo kali. Ikiwa mwanafunzi huyo atakutwa kwa mara ya pili na simu basi huenda akafukuzwa shule.