Kampuni ya Boston Dyanamics imeanza kuuza roboti mbwa anayeenda kwa jina la Spot kwa mtu au kampuni yenye uwezo na uhitaji wa roboti huyo.
Kampuni ya Boston Dyanamics ishawahi kumilikiwa na kampuni ya Google kwa miaka ya 2013-2017 kabla ya kuuzwa kwa shirika la kijapani linaloenda kwa jina la Softbank Group.
Roboti Mbwa Spot ametengenezwa ili kuwa msaada mkubwa katika sekta za ujenzi, uchimbaji madini, na sekta zingine kama hizo. Roboti huyu ametengenezwa katika namna ambayo inakuwa rahisi yeye kuongezewa uwezo spesheli kwa ajili ya kazi spesheli. Mfano anaweza ongezewa mkono mrefu wa kuokota vitu, au pia anaweza kupewa uwezo wa kubeba mizigo mingi zaidi.
Katika sekta za ujenzi na uchimbaji madini roboti huyu anaweza fikia sehemu ambazo zinaweza kuwa ngumu kufikiwa na binadamu. Anaweza tembea sehemu ngumu kupitika na pia anaweza kubeba vifaa vizito kwa umbali mrefu ukilinganisha na binadamu, pia anaweza tumika kutengeneza ramani spesheli za maeneo ya ujenzi.
Bei?
Boston Dynamics wamesema roboti huyu ataanza kupatikana kwa mfumo wa malipo ya awamu – kwa mwezi, ila malipo hayo wamesema ni sawa na malipo ya gari. Kwa sasa kwa wastani gari jipya nchini Marekani ni takribani $37,000 (zaidi ya Tsh 85,000,000/=).
Kampuni ya Boston Dynamics imesema ni lengo lao kuona bei ya roboti huyo ikishuka zaidi. Ila lengo hili linaweza kufanikiwa kama kutakuwa na mahitaji makubwa ya roboti huyu – yaani mauzo mengi zaidi yatasababisha bei kushuka.