Apple watambulisha prosesa mpya za M1 kwa ajili ya kutumika katika laptop zake za Macbook. Kupitia prosesa hii wameweza kutengeneza laptop zenye ufanisi bora zaidi ukilinganisha na kama laptop hizo zingekuja na prosesa za Intel.
Kwa muda mrefu Apple wamekuwa wakitengeneza laptop zao kwa kutumia prosesa kutoka kampuni ya Intel, kwa muda mrefu Apple walikuwa wanaona kama vile prosesa hizo zinashindwa kuendana na uharaka wanaouhitaji kwenye vifaa vyao. Kutokana na kuwa na pesa nyingi, Apple waliwekeza katika tafiti kupitia kampuni inayowatengenezea prosesa zinazotumika kwenye iPhone na iPad – lengo likiwa kuvifanya vifaa hivi kutokuwa tofauti sana kiteknolojia.
Soma -> Mambo 4 Muhimu ya Kufahamu katika Ununuaji wa Laptop
Prosesa ya M1, ambayo ni sehemu ya familia ya prosesa zake za ARM (Apple Silicon) ina sifa zote za kiutengenezaji sawa na zile za kwenye iPhone na iPad. Faida moja wapo iliyopatakana ni ujio wa uwezo wa apps za iPad na iPhone kuweza kutumika kwenye laptop zinazotumia prosesa hiyo. Hili kwa sasa lipo kwenye majaribio ila ni jambo ambalo tulitegemee mbeleni.
MacBook Air
MacBook Air mpya inayokuja na prosesa ya M1 ina ufanisi wa haraka wa mara 3.5 ukilinganisha na toleo lililopita la MacBook Air lililokuja na prosesa za Intel. Pia kutokana na prosesa hiyo inayobeba sehemu zote muhimu za utendaji wa kompyuta (CPU na GPU) umefanya ufanisi wa teknolojia za ‘graphics’ kuwa mara 5 bora zaidi ukilinganisha na toleo lililopita la MacBook Air. MacBook Air mpya zinaanza kwa bei ya takribani Tsh Milioni 2.4.
MacBook Pro
Laptop maarufu kwa ajili ya wazee wa kazi nzito nzito, MacBook Pro ya ukubwa wa inchi 13 nayo imepata toleo jipya linalokuja na prosesa ya M1. Kwa MacBook Pro utumiaji wa prosesa hiyo umefanya toleo hili la MacBook Pro kuwa na ufanisi wa mara 2.8 zaidi (CPU) ukilinganisha na toleo lililopita. Katika eneo la ubora wa teknolojia za muonekano (graphics), ambazo ni muhimu kwa kazi za filamu na picha, toleo hili la MacBook Pro ni bora kwa mara 5 zaidi ukilinganisha na toleo lililopita lililokuja na prosesa ya Intel.
Bei ya MacBook Pro inaanzia takribani Tsh Milioni 3.
———
Hali ipoje kwa kampuni ya Intel?
Intel ni kampuni kubwa duniani kwenye utengenezaji wa prosesa zinazotumika kwenye vifaa vingi vya kompyuta. Kupoteza dili la Apple ingawa haitakuwa habari nzuri ila si kubwa sana kwao kwani kompyuta za Mac bado zinashikilia asilimia ndogo tuu za mauzo yote ya kompyuta duniani kote.
Na ni mtazamo wa wengi ya kwamba Intel angeweza kuboresha kwa haraka prosesa kwa ajili ya Apple ila suala la kuwekeza pesa nyingi kwa wakati biashara yao kwa ujumla bado ni nzuri haikuwapa umuhimu huo. Ila kwa sasa kutokana na laptop hizi kuwa na ufanisi mkubwa basi tayari wateja wao wengine wanaweza wakaanza kudai prosesa za ubora huo na wakawa tayari kuzilipia kwa ajili ya matoleo mapya ya laptop zao; hapa tunaongelea makampuni kama vile ASUS, ACER, HP na mengineyo.
Je ni nani anawatengenezea Apple prosesa zake?
Apple wanasimamia ubunifu wote wa prosesa zao na kisha kuzitengeneza kupitia kampuni ya utengenezaji prosesa ya TSMC ya nchini Taiwan.
Soma habari za Apple -> Teknokona/Apple
Soma -> Mambo 4 Muhimu ya Kufahamu katika Ununuaji wa Laptop
No Comment! Be the first one.