Prosesa za Celeron kutoka kampuni ya Intel zimepata umaarufu sana siku hizi kwani zinakuja kwenye kompyuta/laptop za sifa mbalimbali. Lakini je ni nzuri kwako?
Prosesa za Celeron ni prosesa zilizotengenezwa na Intel zikiwa na sifa ya kuwa za bei nafuu lakini zikilenga kutumika kwenye kompyuta zisizohitaji nguvu nyingi ya utendaji: zinazotumika kwa kazi nyepesi za kikompyuta.
Prosesa ni kifaa kinachopatikana katika kila kompyuta, na ni makampuni mawili duniani ndio yaliyoteka eneo hili, kampuni ya Intel na ya AMD. Ni moja ya kifaa muhimu kwenye kompyuta yako kwani ndicho kinachotafsiri na kuelekeza mambo yote unayoyafanya kwenye kompyuta yako.
Hapa nitaelezea sifa na utofauti wa prosesa za Celeron na zile maarufu za familia ya Pentium kwa lugha ngumu kidogo alafu nitaelezea kwa uwepesi pia.
Celeron za sasa zimetengenezwa kutumia teknolojia ya Pentium 4 core ila ikiwa na ‘chips’ zenye uwezo mdogo wa kukariri taarifa (cache memory) ukilinganisha na zile za Pentium 4. Ata jina lake la kitaalamu zaidi limebeba neno Pentium, wenyewe Intel wakiitambua kama Pentium Celeron. Kingine kinachotofautisha prosesa za Celeron na zile maarufu za familia ya Pentium 4 ni pamoja na uwezo mdogo wa kuhimili kuendelea kufanya kazi kuzidi kiwango chake cha kawaida yaani ‘overclock’. Prosesa za Pentium 4 zimepewa uwezo mkubwa wa kuhimili mzigo zaidi ya kiwango chake cha kawaida.
Kwa uwepesi
Katika kuja na prosesa za familia ya Celeron ni wazo la Intel kuwa na familia ya prosesa zenye gharama nafuu katika utengenezaji ili kuhakikisha uwezo wa kuendelea kuwa na soko kwenye kompyuta za bei nafuu. Prosesa hizi zimetengenezwa kuweza kufanya kazi bila kutumia umeme mwingi na hivyo kuwezesha ata kompyuta zenye uwezo mdogo wa betri n.k kuweza kufanya kazi kwa muda mrefu.
Turudi kwenye mada kuu, je ni kwa kazi za aina gani kompyuta yenye prosesa za familia ya Celeron zinafaa zaidi?
- Kwa kazi za kawaida; Word, Powerpoint na Excel, yaani kazi za kiofisi za kawaida.
- Kwa matumizi ya kutembelea mtandao zaidi (internet browsing) – mitandao ya kijamii, kuangalia video mitandaoni n.k.
Kama unanunua kompyuta/laptop kwa ajili ya matumizi yafuatayo basi epuka kabisa zile zinazokuja na prosesa ya familia ya Celeron:
- Kwa ajili ya kucheza magemu; Magemu ya kwenye kompyuta yanahitaji uwezo mkubwa wa kompyuta hasa kwenye eneo la prosesa. Kama lengo ni hili basi bora uchague kompyuta inayokuja na prosesa za familia ya i5 au i7 kwa familia ya Intel. i3 kama yatakuwa magemu yasiyo ya kisasa sana.
- Kwa ajili ya kutengeneza miziki na video; Kazi kuandaa vipindi vya video au muziki zinatumia programu nzito za kompyuta zinazohitaji prosesa zenye uwezo mkubwa. Celeron haifai kwa kazi hizi.
- Kwa wale wanaofungua na kutumia programu nyingi za kompyuta kwa wakati mmoja. Hili nalo linahitaji prosesa yenye sifa nzuri na kiwango kizuri cha RAM.
Intel wanatengeneza prosesa za familia ya aina mbalimbali wakilenga kompyuta zenye sifa ya uwezo mdogo hadi mkubwa. Kama tungezipanga kuanzia chini kwenda kiwango cha juu basi tungezipanga hivi; Atom, Celeron, Pentium, i3, i5,i7 na Xeon. Kama unavyoona hapo Celeron ipo ya pili kutoka chini kwenye uwezo wake kiutendaji.
Je kompyuta yako inatumia prosesa gani? Je inaendana na kazi zako? Endelea kutembelea Teknokona kujifunza zaidi na kumbuka kusambaza makala kwa wengine.