Changamoto za kiusalama zimekuwa ni moja kati ya matatizo yanayosumbua nchi nyingi duniani kote na hivyo basi kufikiria kuja na njia mpya/bora zaidi ambazo zitahakikisha kuwa changamoto hizo zinakabiliwa kwa haraka na urahisi zaidi.
Kwa asilimia kubwa tu vyombo vya kiusalama (hasa katika nchi zilizoendelea) zinatumia teknolojia ya hali ya juu katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku na hivyo kufanya nchi hizo kukabiliana na uhalifu kwa haraka zaidi. Polisi wa Dubai sasa wameamua kufanyia majaribio pikipiki zinazopaa kabla ya pikipiki hizo kuanza kutumiwa na polisi hao.
Lengo la kufanyia majaribio pikipiki zenye uwezo wa kupaa ni kuboresha namna ya kukabiliana na usalama (ajali za barabarani na uhalifu).
Ufanisi wa pikipiki yenye uwezo wa kupaa.
Pikipiki hiyo ambayo kwa lugha ya kigeni (Kiingereza) inafahamika kama Hover Bike imetengenezwa na kampuni ya Kirusi, Hoversurf inatumia mafuta ya petroli na inaweza kwenda umbali wa 70Kph ndani ya dakika 25 pamoja na kubeba uzito wa mpaka Kg. 300.
Katika majaribio imebainika kuwa Hover Bike ni bora na itasaidia katika kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiusalama, madhalani kufika eneo la tukio ndani ya muda mfupi tofauti na ilivyo sasa. Mbali na kufanyiwa majaribio ya ufanisi wa Hover Bike, pikipiki hiyo pia ilijaribiwa uwezo wa kukabiliana na vumbi/injini kuchemka na matokeo ya jaribio hilo yakawa mazuri.
Polisi wa Dubai wanatarajiwa kuanza kuzitumia pikipiki hizo kufikia mwaka 2020 jambo ambalo kwa hakika litaboresha ufanisi wa kazi kwa Polisi na kuimarisha usalama wa raia na mali zao. Kwa nchi za Afrika, unadhani mbinu hii inaweza kusaidia?
Vyanzo: Gulf News, Telegraph