Wateja wa kampuni ya mawasiliano ya Vodafone nchini Misri wamo mbioni kupata dakika 11 za bure za kuongea kwenye simu.
Kwa mujibu wa tovuti ya 101 Great Goals, zawadi hii itapatikana pale tu mshambuliaji wa Liverpool Mohamed Salah atakapofunga goli katika mechi zilizosalia za msimu wa 2017-2018.
Vodafone ambayo mwaka 2017 iliripotiwa kuwa na wateja 43 milioni nchini Misri, ilitangaza Machi 20, 2018 kwamba kila Salah atakapofunga goli, wateja wake watapewa dakika 11 za kwenye simu ‘Bwerere’. Kampuni hiyo ilichagua dakika 11 kutokana na nambari ya jezi ya Mohamed Salah mgongoni.
Wasifu wa Salah kwenye soka
Salah, 25, mwenye asili ya Misri amefungia Liverpool mabao 28 katika mechi 31 ilizocheza kwenye Ligi Kuu msimu huu. Pia ‘Amemegea’ wachezaji wenzake pasi 10 ambazo zimezalisha mabao.
Vilevile, Salah ameisaidia Liverpool kuingia robo-fainali ya Klabu Bingwa Ulaya baada ya kutikisa nyavu mara sita na kumega pasi mbili zilizozaa goli.
Katika mechi iliyopita, Salah alipachika mabao manne Liverpool ilipoichapa Watford goli 5-0 Machi 17 uwanjani Anfield.
Kwenye Ligi Kuu, Salah anahitaji mabao mawili pekee kufuta rekodi ya mfungaji wa mabao mengi katika msimu mmoja kutoka bara la Afrika; rRaia wa Ivory Coast, Didier Drogba anashikilia rekodi hiyo ya mabao 29 aliyofungia klabu ya Chelsea msimu 2006-2007.
Salah pia anakaribia kufuta rekodi za mabao 34 katika msimu mmoja zilizowekwa na Andy Cole (Manchester United, 1993-1994) na Alan Shearer (Blackburn Rovers, 1994-1995) wakati ligi ilikuwa na klabu 22. Wakati huu, ligi inajumuisha timu 20.
Ratiba ya mechi za Liverpool zilizosalia msimu 2017-2018:
Machi 31 – Crystal Palace vs. Liverpool (Ligi Kuu)
Aprili 4 – Liverpool vs. Manchester City (Robo-Fainali ya Klabu Bingwa mkondo wa kwanza)
Aprili 7 – Everton vs. Liverpool (Ligi Kuu)
Aprili 10 – Manchester City vs. Liverpool (Robo-Fainali ya Klabu Bingwa mkondo wa pili)
Aprili 14 – Liverpool vs. Bournemouth (Ligi Kuu)
Aprili 22 – West Brom vs. Liverpool (Ligi Kuu)
Aprili 28 – Liverpool vs. Stoke (Ligi Kuu)
Mei 5 – Chelsea vs. Liverpool (Ligi Kuu)
Mei 13 – Liverpool vs. Brighton (Ligi Kuu)