Kasi katika matumizi ya kompyuta ni muhimu kwa maisha ya sasa. Huwezi kujisikia raha pale unapotaka kuandika hati ya muhimu kwenye kompyuta ikakuchukua dakika kadhaa kufungua programu ya kuandikia au kutaka kusikiliza muziki kwenye simu-janja ikakuchukua muda mrefu mpaka hamu ikakuishia.
Bila shaka umewahi kujiuliza kwa nini kompyuta yako au simu hupungua kasi. Sababu kuu zinazofanya kompyuta kupungua kasi ni kuongezeka kwa ‘data’, kiasi cha programu zinazofanya kazi kwa wakati mmoja, pamoja na uchakavu wa programu au mfumo-endeshaji wa kompyuta unayoitumia (‘operating system’) . Kurudisha kasi ya kompyuta au simu yako, hauna budi kuyakabili matatizo haya.
Punguza kuongezeka kwa Data
Inawezekana una mazoea ya kujaribu programu tofauti na kuziacha kwenye kitumi chako bila ya kazi, mpaka unajikuta umepakia programu nyingi kupitiliza. Hili ni tatizo kubwa! Programu hizi huhifadhi mambo kibao usioyahitaji kwenye kitumi chako na pia hutumia rasillimali kubwa ambazo zingeweza kutumika na programu nyingine unazoziitaji zaidi.
Kuleta mabadiliko na kuongeza kasi, hakikisha unafuta na unaacha programu zile tu ambazo unatumia mara kwa mara. Kufuta, futa programu kwa kutumia programu zingine maalum kama ‘Clean Master, ya Android‘ na ‘Wise Disk Cleaner‘ ya Windows, ambazo pamoja na kufuta programu, huondoa pia mazagazaga mengine yanayopunguza kasi ya kifaa chako.
Punguza Kiasi cha programu zinazofanya kazi kimya-kimya na kwa wakati mmoja
Njia ya pili ya kuongeza kasi ya kompyuta yako ni kupunguza programu zinazofanya kazi kimya kimya. Hizi ni zile zinazoanza pamoja na mfumo wako, zile zinazotumia mtandao kuji-‘update’ na zile zinazosubiria uzitumie tena (‘cached’, kwa lugha ya kitaalamu). Wakati unatumia kifaa chako, jaribu kuzima kila programu unayomaliza kutumia au tumia programu maalum ambazo zitafunga hizo programu, kama ‘Advanced Task Cleaner‘ ya android. Punguza kutumia ‘synchronization’ na ‘widgets.’ Hizi ni programu hasa kwenye mifumo ya android ambazo hufanya programu kuendelea kufanya kazi hata kama huzitumii.
Pia, jaribu kuzima programu zinazoanza na mfumo wako kupitia mipangilio (‘settings’) ya mfumo wako. Kwa mfano kwenye mfumo wa windows, tafuta jinsi ya kupangilia ‘start-up applications.’ Ukiweza kuzima hizi programu, utaiwezesha kompyuta kuwaka kwa kasi zaidi. Sababu kuu ya tatu ya kifaa chako kupungua kasi ni uchakavu wa programu ulizokuwa nazo na mfumo wa kompyuta.
Watengenezaji wa mfumo wa kompyuta na programu unazotumia hutoa marekebisho kadhaa almaarufu kama ‘updates’ kila baada ya muda. Ni vyema kujenga tabia ya ku-‘update’ programu zako ili upate kasi zaidi na manufaa mengine kama usalama zaidi, urahisi wa utumiaji na huduma mpya.
Pakia upya mfumo wa kompyuta yako.
Jambo la mwisho linaloweza kwa kiasi kikubwa sana kuongeza kasi ya kompyuta yako ikiwa njia zote zimeshindikana, ni kupakia upya mfumo wa kompyuta yako. Ukiamua kufanya hili basi kuwa makini. Huna budi kufanya maandalizi ya makini. Hifadhi data zako kwanza.
Kupakia mfumo wa kompyuta hufuta kila kitu kwenye kompyuta yako. Ukiweza kupakia mfumo wako upya utakuwa umendoa pia kila aina ya programu ulizowahi kupakia kwenye kompyuta yako na hivyo utakuwa umeondoa uchafu wote uliokuwa kwenye kompyuta yako na kuanza upya. Hii itaifanya kompyuta yako kufanya kazi kama vile ndio kwanza imetoka kiwandani!
Ningependa mnipe maelezo ya kina kuhusu simu jamja aina ya Tecno CX