Kila mmiliki wa tovuti ya biashara leo hii anajua ni kwa namna gani ilivyo rahisi kuanzisha biashara mtandaoni.
Lakini kama uko katika sekta ya masoko mtandaoni kwa miaka kadhaa sasa, unaweza kuwa na dondoo ni kwa namna gani kazi ilivyo ngumu katika kudumisha uhai wa tovuti za aina hiyo.
Unapaswa kuendana na kasi ya mabadiliko ya tovuti injini za kutafuta taarifa mpya na pia kubaki salama dhidi ya matapeli, kunakiliwa bila ruhusa kwa kazi mbalimbali na matatizo yanayoletwa na wadukuzi.
Katika biashara, wateja huchukuliwa kuwa ndiyo uti wa mgongo kwa sababu hiyo, kuiweka biashara yako salama dhidi ya mashambulizi hatari kama ya wadukuzi ni jambo muhimu.
Je, ni jinsi gani utaiweka huru biashara yako dhidi ya mashambulizi mtandaoni? Sasa fahamu njia 7 zinazoweza kuiepusha biashara dhidi ya hatari za mtandaoni:
1. Sajili nembo/jina la biashara yako.
Kitu cha kwanza ambacho mmiliki wa biashara lazima akifikirie ni kuhakikisha kwamba jina la kampuni yake limesajiliwa rasmi kibiashara.
Haitoshi peke yake kupata jina la utambulisho wa tovuti (domain) na kuanzisha kampuni, bali unapaswa pia kulinda jina la biashara yako. Hili litakulinda na wavamizi, ‘Wazee wa kunakili’ na yeyote atakayetaka kujinufaisha kupitia chapa yako.
2. Weka tovuti yako katika jukwaa la kuaminika.
Majukwaa bora ya biashara za mtandaoni, ni Spotify na BigCommerce ambapo wamiliki wengi wa tovuti za biashara huzitumia hizo mbili zaidi.
Kama ukitumia majukwaa hayo, utapaswa kuwalipa watu wakutengenezee ‘stoo’ yake na kusimamia vigezo vya kiusalama. Mtoa huduma za mtandao aliye mzuri atahakikisha kwamba stoo yake ni salama dhidi ya vitisho wakati akipata suluhu ya majibu dhidi ya matatizo yatakayojitokeza.
3. Tumia Soketi Salama (SSL).
Hizi SSL (Secure Sockets Layer) huchukuliwa kama kiwango cha kupima teknolojia ya usalama katika viungio (links) baina ya kivinjari na kihifadhi cha tovuti.
Kiungio cha habari isiyotafsiriwa (encrypted) itahakikisha kwamba taarifa zako zinasambazwa kwa ajili yako tu. SSL ni muhimu kwa kila muamala wa biashara ya mtandao kwa sababu zinasaidia kulinda taarifa binafsi za mtu na pia taarifa nyeti za kifedha katika mchakato mzima wa manunuzi mtandaoni.
4. Zingatia na kuzifuata kanuni za malipo salama ya manunuzi mtandaoni (PCI DSS).
Tovuti za biashara mtandaoni lazima zikidhi vigezo vya PCI DSS ili kuchakata malipo kwa usalama. Vitangamanishi vya malipo kama Braintree na Stripe vina uwezo wa kufumba na kuhifadhi taarifa binafsi za kadi yako ya malipo. Matokeo yake, taarifa nyeti za malipo hazitunzwi katika tovuti yako.
5. Hakikisha unaiboresha tovuti yako mara kwa mara.
Kinachozifanya tovuti za biashara kuwa dango rahisi la uhalifu wa kimtandao ni kule kutoboreshwa mara kwa mara, hasa kwa programu tumishi. Mfano, kwa kutegemea tu uboreshwaji rahisi kupitia programu maalum iitwayo ‘web crawler’ inakuwa rahisi kwa wadukuzi kuvamia tovuti husika.
6. Weka nywila (nenosiri) za kipekee.
Wadukuzi hutumia mchanganyiko wa namba na herufi kuvamia nywila za tovuti. Ili kuzuia wadukuzi kufikia kanzidata (database) yako hakikisha unakuwa na nywila madhubuti zilizo na ziada ya tabaka za mifumo ya kiulinzi.
7. Tambua nyendo za wahalifu.
Njia bora zaidi ya kudhibiti uhalifu ni kujua viashiria vyake. Kuwa macho na majina ya barua pepe, historia za wateja katika uagizaji bidhaa na pia majina ya tovuti zao.
Wahalifu kwa kawaida huzilenga bidhaa za thamani kubwa. Mara zote fuatilia ‘data’ za wateja na taarifa zao nyingine zilizo muhimu.
Nyongeza ya yote, tambua kuwa wafanyakazi wana nafasi kubwa ya kulinda biashara dhidi ya uhalifu wa mitandaoni. Elimu sahihi na ya kutosha kuhusiana na usalama mitandaoni itasaidia kwa kiasi kikubwa mapambano dhidi ya wahalifu wa mtandaoni. Unaweza kupata mafunzo mengi yanayokidhi mahitaji ya biashara yako.
Bado hatuna takwimu nzuri kwa hapa Tanzania kuna tovuti ngapi zinazouza bidhaa na kumuwezesha mteja kununua kwa kufanya malipo moja kwa moja kwa njia ya mtandaoni kama tovuti maarufu za Ebay, Amazon, AliExpress na zinginezo.