Nichague Mtandao Upi kwa ajili ya matumizi ya intaneti? Hili ni swali ambao wengi wanajiuliza mara nyingi pale wanapotaka kununua vifaa vya huduma ya intaneti kutoka makampuni ya simu kama vile modemu, MiFi au ruta.
Na saa nyingine unajiuliza suala hili kama unamiliki simu janja yenye mahitaji mengi ya huduma ya intaneti ya uhakika.
Je uchague mtandao gani kati ya Airtel, Tigo, Vodacom, Zantel, Halotel na mingine mingi mipya inayokuja?
Nachotaka kukuhakikishia ni kwamba ingawa utaambiwa mtandao fulani ndio kasi zaidi ya mwingine flani kuna uwezekano mkubwa ukachagua mtandao unaosifiwa ila ukafika kwako ukakuta huduma ipo ‘slow’ kuliko kawaida na ukashangaa kuona mtandao uliokuwa unapondwa ndio upo kasi zaidi.

Kikubwa cha kutambua tukiweka pembeni mitandao inayotoa huduma ya intaneti kwa mfumo wa 4G pekee kama vile Smile na Smart kwa mitandao mingine hawana tofauti sana katika teknolojia zao ila kikubwa ni utofauti wa maeneo waliyopo na jinsi gani unapata signal zao hapo ulipo. Pia wingi wa minara yao na ukilinganisha na idadi ya watu inayowapatia huduma hiyo.
Ingawa kwenye matangazo ya kibiashara watatangaza ya kwamba wapo karibia nchi nzima kwa teknolojia ya zaidi ya 3G ukweli ni kwamba utakapokuwa unatumia utagundua kuna maeneo mengi ata yaliyo mijini ambayo utashindwa kupata huduma ya intaneti katika mfumo wa 3G na kama ukiwa kwenye 3G basi spidi yake itakuwa ndogo kiasi cha kuleta ata mauzi.
Kuna sehemu utakuwepo na utakuta katika mitandao yote mikubwa ni mmoja tuu ndio unakupa signal za 3G ambayo ni kasi kulinganisha na ya 2G/EDGE. Na pia unaweza ukakuta baadhi ya sehemu unapata kweli signal za 3G lakini bado huduma ya intaneti ipo taratibu sana.
Hivyo ufanyaje katika kuchagua?
Hatua ya kwanza ulizia wengine walio katika eneo husika kama vile maeneo ya kwenu ambapo utakuwa unatumia huduma hiyo ya intaneti zaidi. Ulizia kwa watu wanaotumia mitandao tofauti na wakueleze kama huduma ya intaneti kwao inasumbua na kama ipo poa basi je ni kwa spidi gani.
Hatua ya pili, hii ni kama inawezekana. Jaribu kuona kama mitandao hiyo inafanya vizuri ata ukiwa ndani ya nyumba au ofisi ya hapo utakapokuwa unatumia huduma hiyo. Hii ni muhimu kwani kuna maeneo mengine ‘signal’ zinakuwa hazina nguvu kabisa kifaa kikiwa ndani ya jengo.
Hatua ya tatu, pitia matangazo yao kuhusu bei za vifurushi vyao na angalia vizuri ni mtandao upi kati ya hiyo inayofanya fanya kazi vizuri eneo ambalo utakuwa unatumia kifaa chako una vifurushi na bei nzuri zaidi kwako.
Ukipitia hizo hatua tatu hakika hautanunua kifaa au kulipia kifurushi cha intaneti na kisha kujuta uamuzi huo kutokana na kushindwa kufurahia huduma kutoka mtandao husika.
Soma – Fahamu Tofauti Kuu Kati ya Teknolojia za 2G, 3G, 4G n.k
Pia kuna jambo moja ambalo linaweza lisiepukike, mwenyewe lishanikuta na nikakasirika sana. Unaweza kununua kifaa cha bei ghari kama vile ‘Router’ na siku moja ukaama makazi na ukajikuta ulipo amia huduma ya mtandao husika unaoutumia ni mbovu balaa, hili haliepukiki linaweza kutokea cha kufanya kama haupo tayari kubadilisha mtandao mara kwa mara basi pia uwe unachunguza kuhusu upatikanaji wa huduma za intaneti katika maeneo husika wakati unatafuta ofisi au makazi mapya.
Je katika eneo lako la kazi au makazi ni mtandao gani unasifika zaidi katika ufanisi kwenye eneo la intaneti?
No Comment! Be the first one.