Kampuni ya Netflix mwishoni mwa wiki iliyopita ilipandisha bei ya baadhi ya vifurushi vyake kwa watumiaji wa Marekani. Mabadiliko hayo ambayo wenyewe wanasema hayaji kwa uharaka katika mataifa mengine yanaonekana yamekuja katika kipindi ambacho tayari kuna ushindani mkubwa nchini humo kutoka huduma zingine kama vile Apple TV, Amazon Prime na nyingine nyingi.
Vifurushi vilivyopanda bei ni kile cha standard ambacho kwa sasa kitakuwa kinauzwa Tsh 32,456 ($13.99) na kile cha premium ambacho kitauzwa Tsh 41,736 ($17.99) Kabla ya mabadiliko haya kifurushi cha standard kilikuwa kinauzwa kwa gharama ya Tsh 30,136 ($12.99) wakati kile cha premium kilikuwa kinauzwa kwa Tsh 37,096 ($15.99).
Mabadiliko haya ni kwa watumiaji waliosajiliwa katika soko la Marekani. Msemaji wa Netflix amesema kwamba mabadiliko haya ya bei kwa Marekani, hayaleti ushawishi ama hayaoneshi kwamba bei zitabadilika katika masoko mengine.
Kwa faida ya wale wasiojua, Netflix wana vifurushi vitatu ambavyo watumiaji wanaweza kuchagua:
Basic; Hiki ni ndio kifurushi cha bei rahisi kuliko vyote, unalipa Tsh 20,856 ($8.99) unaruhusiwa kutumia katika kifaa kimoja tu kwa wakati mmoja na ubora wa picha wa kiasi cha chini kabisa. Kifurishi hiki kinawafaa watu ambao hawana wategemezi, maana huwezi kutumia akaunti yako kama kuna kifaa kingine kinatumia akaunti hiyo.
Standard; Hiki kifurushi cha bei ya kati, unalipa Tsh 32,456($13.99)(bei ya zamani ilikua Tsh 30,136) unaweza kutumia katika vifaa viwili kwa wakati mmoja na ubora wa picha ni wa HD. Kifurushi hiki kinawafaa watu wenye angalau mtegemezi mmoja, mkiwa wawili mnaweza gawana gharama na mkalipia kifurushi hiki.
Premium; Kifurushi hiki ambacho kinauzwa Tsh 41,736, kilikuwa kinauzwa Tsh 37,096 kabla ya mabadiliko. Kifurushi hiki kinakupa pamoja na mengine ubora wa picha bora kama 4HD na 4k, pia kinakuruhusu kufungua Netflix walau katika vifaa vinne kwa wakati mmoja.
Bei hizi mpya zitaanza kulipwa baada ya miezi miwili. Watumiaji wa Netflix walio katika vifurushi vyenye bei mpya watapatiwa tangazo walau siku 30 kabla ya bei mpya kuanza.
Je wajua kwamba Netflix ilipoanzishwa mwaka 1998 ilikuwa inasambaza video kwa kutumia DVD, mfumo huu wa mtandao unatumika kwa sasa ulianza mwaka 2007.
No Comment! Be the first one.