Hatimaye Andy Rubin mmoja wa waanzilishi wa mfumo endeshi wa Android ametegua kitendawili chake kwa kuzindua Simu Janja kama alivyoashiria siku chache zilizopita.
Andy Rubin aliyeondoka kampuni ya Google mwaka 2014, na kuanzisha kampuni yake ya inayojulikana kama Essential Products Inc, amezindua simu yake ya kwanza ya kiwango bora na kinachokubalika kimataifa.
Hata hivyo haijajulikana simu hiyo kama itaweza kuvunja soko kubwa la utawala wa Samsung na Apple. Kwa mujibu wa kampuni ya utafiti na uchambuzi ya Gartner kwamba mauzo ya simu za samsung ni asilimia 21 na Apple asilimia 14 ya simu zote duniani.
Andy Rubin katika uzinduzi wa Simu hiyo ya Essential uliofanyika huko California, nchini Marekani alisema anaamini simu yake italeta ushindani mkubwa na hata kuwapiku magwiji hao katika soko la simu duniani.
Alisema simu hiyo itaanza kuuzwa muda mfupi ujao kuanzia marekani na sehemu zingine za dunia. Itagharimu kiasi cha Dola 699 za kimarekani.
Essential imeundwa kwa madini ya Titanium na kuifanya Housing yake kuwa ngumu hivyo kuifanya simu hiyo kutohitaji mfuniko maalumu wa kuikinga na kuvunjika na sehemu kubwa ya mbele ikijazwa na kioo.
Aidha itakuwa na kamera mbili za nyuma na moja yenye uwezo wa kuchukua picha hata katika mazingira yenye mwanga mdogo. Andy Rubin anasema simu hiyo haitakuwa na jina juu yake au logo bali muonekano wake utatosha kumjulisha mtu ni simu ya aina gani.
Simu hiyo bado haijawekwa wazi itakuwa na mfumo endeshi wa Android ama la. Kuna tetesi inaweza kuja na mfumo endeshi unaojulikana kama Ambient.
Sifa zingine ni kwamba Inakuja na kioo cha ukubwa wa inchi 5.7 (2,560×1,312), Diski uhifadhi (storage) ni 128GB. Kiwango cha ni RAM 4GB na Ukubwa wa Betri ni 3,040mAh.
Itakuwa na prosesa ya 2.4GHZ octa-core Qualcomm Snapdragon 835, Kamera za nyuma 13-megapixel(RGB) na 13-megapixel(monochrome) na Kamera ya nyuma 8-mega pixel.