Mwalimu mmoja wa somo la ICT (Information and Communication Technology) nchini Ghana ametambuliwa katika ulimwengu kwa madhira anayopata katika ufundishaji wa somo hilo la mambo ya elimu ya kompyuta kwa wanafunzi wake.
Kwa kawaida somo hilo hufundishwa kwa nadharia na vitendo ambapo vitendo ni lazima kuwepo na Kompyuta ili wanafunzi waelewe kinachofundishwa. Mwalimu Richard Appiah Akoto anafundisha programu ya Microsoft Word kwa kulazimika kuchora ubaoni na kutumia chaki za rangi tofauti ili somo lake lipate kueleweka kwa wanafunzi.
Shule hiyo iliyo na miaka 14 tangu kuanzishwa kwake haijawahi kuwa na kompyuta ya aina yoyote shuleni hapo. Wanafunzi wake wanatarajia kufanya mtihani wa taifa na moja ya mtihani utakaowafanya kufaulu kwenda elimu ya sekondari ni wa ICT ambapo kama watafeli hawataruhusiwa kujiunga na sekondari.
Mwalimu Akoto alituma picha zake mwenyewe katika akaunti yake ya Facebook akionesha anavyojaribu kuelezea Kompyuta licha ya kutokuwa na Kompyuta halisi. Akoto anasema sio mara ya kwanza kufundisha Microsoft Word kwa kuchora ubaoni, amekuwa akifanya hivyo tangu alivyoanza kufundisha shuleni hapo.
Akoto ana kompyuta yake binafsi lakini haitumii kufundisha katika darasa kwa sababu anahitaji kuwa na kompyutaza mezani (Desktop) ambapo atawaelekeza namna ya kuunganisha kifaa kimoja baada ya kingine mfano Mouse, Keyboard, Monitor, n.k kama mtaala wasomo husika unavyoeleza.