MP 108, yaani Megapixel 108… zote hizi ziwe kwenye simu janja yako mkononi. Kampuni nguli katika utengenezaji wa simu na vifaa vya simu ya Samsung imetambulisha rasmi kipuli cha kamera ya simu janja cha megapixel 108.
Wiki hii, jumatatu, kampuni ya Samsung ilitambulisha rasmi kamera ya simu yenye uwezo wa kupiga picha za zaidi ya megapixel 100. Hii ni kamera ya kwanza kwa ajili ya simu kuwa na uwezo huo.
Kupitia kamera hii, picha zenye ubora wa hali ya juu zitaweza kupigwa ata sehemu zenye mwanga mdogo zaidi ukilinganisha na kamera za sasa kwenye simu zetu. Pia kamera hii itakuwa na uwezo wa kupiga hadi picha za kiwango cha ubora wa 6K. 6K ni kiwango cha juu cha ubora wa picha kwa sasa, kumbuka kuna viwango mbalimbali vya HD kutoka chini hadi juu ni kama ifuatavyo 720p, 1080p, 4K na 6K.
Wastani wa kamera za sasa kwenye simu janja nyingi duniani ni kati ya megapixel 12 hadi 16. Ni kamera chache sana kwenye simu zina megapixel nyingi zaidi ya hizo.
Katika utengenezaji wa kamera hii inayokwenda kwa jina la Isocell Bright HMX kampuni ya Samsung imeshirikiana na kampuni ya kichina ya Xiaomi na inategemewa simu kutoka Xiaomi ndio itakuwa simu ya kwanza kuja na kamera hiyo hivi karibuni.
Kupitia kamera hiyo, video za ubora wa 6K zinaweza kurekodiwa kwa wastani wa fps (frame per second) 30, huku za ubora wa 4K zinaweza rekodiwa kwa wastani wa fps 60.
Kampuni ya Samsung imejikuta inawekeza zaidi katika vipuli vya simu janja na kuuza kwa makampuni cha nchini China kutokana na kampuni hiyo kupitwa vibaya sana kwenye soko la simu janja nchini humo. Kwa sasa Samsung kwa nchini China inashikilia soko la simu janja kwa asilimia moja tuu, huku makampuni kama Huawei, Xiaomi na Oppo yakishika asilimia kubwa la soko la simu janja nchini humo.