Kwa mara ya kwanza kampuni ya Microsoft imesema hadharani kwamba rasmi sasa hawatatengeneza wala kuendeleza tena mfumo wa Windows kwa simu janja (windows Phone OS).
Taarifa rasmi kupitia mtandao wa Twitter imeelezwa kuwa haina mpango wala matumaini yoyote ya kuongeza matoleo mapya kwa simu zenye programu endeshi ya Windows ambazo miaka ya nyuma zilitokea kupendwa kwa kiasi chake.
Microsoft haitengenezi tena simu zenye kutumia mfumo endeshi wa Windows lakini itaendelea kutoa masasisho kwa programu tumishi zake ili kuimarisha uliznzi wa simu za Windows. Mwaka mmoja uliopita (2016) Microsoft iliacha rasmi utengenezaji wa simu za Lumia.
Sababu kubwa ya kushindwa kwa Mfumo wa Windows Phone ni kukosa watengenezaji (Developers) wengi wa App na hata wale ambao wameweka App zao hawazifanyii masasisho (Updates) tofauti na ilivyo katika Android na iOS.
Simu za Windows zina watumiaji wachache sana na hivyo kufanya kampuni kukosa mapato yatokanayo na simu hizo na hiyo kufanya vibaya kiujumla.
Jambo hilo limechangia sana kupungua kwa watumiaji wa Windows Phone na hivyo kupelekea hasara kwa kampuni ya Microsoft. Kulingana na takwimu za mwaka huu kwamba asilimia 99 ya watumiaji wa simu janja wanatumia zenye mfumo wa iOS na Android na asilimia moja ni Windows.