Serikali inachoifanyia Huawei si sawa, hayo ni maneno ya mmoja wa kiongozi wa juu kabisa ndani ya kampuni ya Microsoft .
Rais wa kampuni hiyo na ambaye pia ni mwanasheria mkuu wa kampuni hiyo bwana Brad Smith alisema hayo alipokuwa katika mahojiano na chombo cha habari cha Bloomberg. Bwana Brad amesema jambo ambalo serikali hiyo inafanya dhidi ya Huawei ni jambo ambalo halina sifa ya misingi ya taifa la Marekani.
Bwana Brad amesema serikali ya nchi hiyo imeshindwa kutumia misingi ya kimahakama ya kushtaki na kuleta mbele ushahidi dhidi ya shutuma zake dhidi ya Huawei na pia kuipa kampuni hiyo nafasi ya kujitetea.
Amesema kwa sasa kila wakizungumza na serikali ya nchi hiyo juu ya zuio linalowahusu wao pia la kufanya biashara na Huawei jibu wanalopata ni ‘mngejua tunachojua, mngekubaliana na sisi’ ambapo Microsoft na wadau wengine wamekuwa wakitoa majibu ya ‘basi tuonesheni hicho mnachojua ili nasi tuwe na uelewa mzuri’ lakini hadi sasa serikali na vyombo vya usalama havijawapa ushahidi wowote wa ubaya wa Huawei.
Suala la Huawei kuwa katika nafasi ya mbele zaidi katika teknolojia ya 5G ni mwiba mkubwa kwa vyombo vya usalama vya mataifa ya magharibi.
Teknolojia ya 5G inategemewa kuwa muhimu sana katika sekta zote muhimu za uchumi na hivyo kumaanisha kampuni ya Huawei kama itauza vifaa na kufunga mitambo kwenye mataifa mengi basi itakuwa ni moja ya makampuni yenye nguvu sana katika sekta nzima ya mawasiliano na usalama wa kidigitali.
Hofu kubwa kwa Marekani ni kwamba jambo hili linaweza kutumiwa kwa ukaribu na serikali ya China katika kudukua data mbalimbali – za kiuchumi, kiusalama na ata za kisiasa za mataifa ya magharibi kama yatatumia vifaa vya 5G kutoka Huawei.