Tayari tumekwisha aandika mara kadhaa juu ya App ya Messenger na ile ya Facebook kusababisha simu kuisha chaji haraka na kuwa nzito ama kupunguza uwezo wa simu kufanya mambo kadhaa.
Ukweli ni kwamba tayari wachambuzi na mitandao mingi ya teknolojia imekwisha andika juu ya tatizo hili. Facebook wameamua kuleta Messenger Lite kwa watumiaji ambao wanasimu zisizo na uwezo mkubwa.
Kuna tofauti gani kati ya Facebook Messenger na Messenger Lite?
Tofauti ni kwamba app tukiyoizoea ya Messenger ina vitu vingi kitu ambacho kinasababisha simu isiyo na uwezo mkubwa ama isiyo na nafasi kubwa ya diski kushindwa kufanya kazi kwa ufasaha, kutatua tatizo hili Facebook wameleta app ambayo itakuwa na mambo ya muhimu tuu ili kuwaruhusu watu ambao wanatumia simu za kawaida kuweza kuitumia bila shida yeyote.
App ya kawaida ya Facebook Messenger ina ukubwa wa zaidi ya MB 50 katika upakuaji wake wakati app hii ya Messenger Lite inachukua chini ya MB 10 tuu.
Pia Messenger Lite haitakuwa inafanya kazi kama haujaifungua – ‘background process’, na pia app haijiwashi na kuanza kufanya kazi yenyewe tuu pale simu inapowashwa. Hii ina maanisha haitakuwa inatumia chaji ya simu yako kabisa pale ambapo hautumii.
Facebook wameleta app hii kwa kuwa wanatambua bado kuna watumiaji wao wengi ambao wanatumia simu janja ambazo zina kiwango cha chini.
Je utakosa nini katika Messenger Lite ambacho kipo kwenye ile app kuu?
- Hautaweza kutuma taarifa ya eneo uliopo – yaani ‘Location’ kwa huduma ya GPS
- Pia uwezi kutuma vile vipicha vya kikatuni, yaani ‘stickers‘ zinazopatikana kwenye huduma zote za kuchati za Facebook – kwenye tovuti na kwenye app ya Messenger. Ila utaweza kuona stika unazotumiwa na watu. Ila pia utaweza kutuma na kupokea picha.
- Kikuu zaidi ni kwamba hautaweza kupiga simu za Facebook, kupitia app kuu ya kuchati ya Messenger mtumiaji anaweza mpigia mwingine bure kabisa kama vile kwenye huduma ya WhatsApp.
Hii ni moja kati ya hatua za kampuni hii kujaribu kuifanya Messenger kuwa ni app inayotumiwa zaidi na wamiliki wa simu janja hasa hasa kwenye nchi zinazoendelea ambapo ukubwa wa Messenger na ulaji wake chaji ulikuwa tayari ni tatizo.
Soma Pia;
- App ya Facebook, Inakula chaji 20% zaidi na Inafanya simu yako kuwa nzito
-
App ya Metal, Tumia Facebook bila simu kuishiwa chaji
Messenger Lite inapatikana soko la Apps la Google kwa nchini chache tuu kwa sasa, wanazidi kuongeza zingine-> Google PlayStore, kama ikikataa kupakuliwa kupitia Google PlayStore basi soma makala yetu – Kuweka Apps kwenye Simu za Android bila Kutumia Google Play na kisha pakua faili la App hiyo (APK) kutoka hapa -> APK Mirror na uinstall kwenye simu yako bila kupitia Google PlayStore.