Mbuzi kutoa maziwa yenye dawa dhidi ya ugonjwa wa kansa – saratani. Haujakosea kusoma. Kichwa cha habari kipo sahihi kabisa. 😀
Wanasayansi wamefanikiwa kubadilisha vinasaba vya mbuzi na kuwezesha miili ya mbuzi hao kutengeneza dawa dhidi ya saratani ambayo itakuwa inapatikana kupitia maziwa yao.
Wameweza kuwafanya mbuzi watengeneze dawa aina ya cetuximab kupitia mfumo wao wa utengenezaji maziwa. Dawa ya Cetuximab inatumika katika matibabu ya saratani ya utumbo zaidi ila pia inaweza kutumika kwenye matibabu ya saratani ya mapafu na za aina nyingine pia.
Utafiti huo umefanikishwa na kikundi cha wanasayansi katika chuo cha utafiti wa AgResearch nchini New Zealand.
Dawa hizo zinazohusisha protini, kawaida kwa utengenezaji wa viwandani dawa hiyo inakuwaga ya gharama ya juu sana. Kwa matibabu inaweza mgharimu mtu hadi zaidi ya milioni 26 kwa mwezi kupata huduma inayohusisha utumiaji wa dawa hizo. Wanasayansi hao wanaamini kwa mfumo mzima wa utengenezaji kufanyika kupitia mbuzi utashusha gharama za dawa hizo kwa kiasi kikubwa sana.
Tofauti na dawa zingine ambazo zimekuwa zinahusisha utengenezaji unaohusisha mashine na kemikali, dawa hizo hadi sasa zimekuwa zinatengenezwa kwa njia ya taratibu sana na inayohusisha gharama nyingi sana za kimaabara. Kutokana na hilo ndio maana bei yake imekuwa juu sana, kwa kutumia Mbuzi dawa itatengenezwa kwa wingi na ndani ya muda mfupi.
Kwa sasa wanaendelea na uchunguzi wa kufahamu kiwango na ubora wa dawa hiyo. Kabla ya kuchukua hatua zaidi za upatikanaji wa vibali na mambo mengine yanayoweza kuwezesha njia yao kupata baraka kutoka vyombo vya juu vya usimamizi wa madawa.
Soma makala za sayansi na teknolojia katika sekta ya afya -> TeknoKona/Afya