Mauzo ya simu yashuka. Robo ya kwanza ya mwaka 2019 ya mauzo ya simu duniani imeonesha kushuka kwa kiwango cha jumla ya asilimia 6.6 kutoka simu 332.7 milioni kwa robo ya kwanza ya mwaka 2018 hadi simu 310.8 milioni kwa robo ya kwanza ya mwaka 2019 kwa mujibu wa ripoti ya IDC (International Data Corporation).
Hii ni tofauti na ilivyozoeleka miaka ya nyuma kwamba mauzo ya simu yalikuwa yakiongezeka mwaka hadi mwaka. Kampuni mbili kubwa za Apple na Samsung zimeshuka kwa mauzo katika robo ya kwanza ya mwaka. Apple wameshuka kwa 30.2% kwa kuuza Simu milioni 36.4 huku Samsung wakishuka kwa 8.1%.
Kampuni ya Huawei kutoka Uchina imeshuhudia kupanda kwa mauzo yake ya simu katika robo ya kwanza ya mwaka kwa 50.3%. Hata hivyo, kampuni ya Samsung imeendelea kushika nafasi ya kwanza kwa mauzo katika robo ya kwanza ya mwaka kwa kuuza Simu 71.9 milioni.
- Nafasi ya pili imeshikiliwa na Huawei kwa kuuza Simu 59.1 milioni na nafasi ya tatu ni kampuni ya Apple ambapo wameuza simu 36.4 milioni.
- Nafasi ya nne imeenda kwa kampuni ya Xiaomi iliyouza simu milioni 25 ikiwa imeshuka mauzo yake kwa 10.2%.
- Nafasi ya tano imeshikiliwa na kampuni mbili ya Vivo iliyouza Simu milioni 23.2 na OPPO iliuza Simu 23.1 zote za Uchina.
Watafiti wengi wanaona kuna uwezekano mkubwa wa Huawei kushika nafasi ya kwanza kuipiku Samsung ndani ya mwaka mmoja hadi miwili kama kasi yao ya sasa itaendelea. Njia pekee ya Samsung kuendelea kushika nafasi ya kwanza ni kufanya mabadiliko makubwa ya kimauzo.
Mauzo ya simu za iPhone kutoka Apple yanaendelea kuporomoka, ni hivi karibuni tuu Apple wametoa taarifa ya kwamba wanaacha kuripoti mauzo ya simu zao katika ripoti zao rasmi. Kwa sasa watakuwa wanatoa ripoti za simu za iPhone zinazotumika – hii ikiwa ni njia ya kutaka wawekezaji wao kujali zaidi mapato wanayopata katika watumiaji wa iPhone waliopo kuliko ata mauzo mapya ya iPhone.
Simu za Huawei zinaendelea kufanya vizuri kwenye masoko mengi duniani – hii ikiwa ni pamoja na China na bara la Ulaya. Simu za Huawei hazipatikani kwa mauzo ya kawaida ya mitandao ya simu nchini Marekani – tofauti na wengine.