Data za mauzo ya kamera zinaonesha ya kwamba utengenezaji na mauzo ya kamera za kawaida yanazidi kuporomoka kutokana na ukuaji wa mauzo na utumiaji wa simu janja.
Miaka kadhaa nyuma ilikuwa ni kawaida kuona mtu anatembea na kamera (Compact Camera) kwa ajili ya kupiga picha kadhaa popote aendapo, siku hizi watu hutumia simu janja (smartphones) zaidi katika kukamilisha hili.
Data za mauzo ya kamera zinaonesha ya kwamba wakati mauzo ya kamera yakizidi kuporomoka ni mauzo ya kamera za kwa ajili ya kutumika kwenye simu ndio yanazidi kukua.
Kwa undani zaidi data hizi zinaonesha ya kwamba ukuaji wa uhitaji wa kamera kwa ajili ya simu janja ndio ulizidi kuua mauzo ya kamera za kawaida.
Simu janja nyingi za kisasa zimeweza kufanikisha upigaji picha wa kiwango cha juu na hivyo watu wengi wamejikuta hawaoni umuhimu wowote wa kununua kifaa kingine kama kamera kwa ajili ya kumilisha itaji lile lile ambalo simu janja zinakamilisha.
Ni kawaida kuona simu janja nyingi kwa sasa kuweza kupiga picha zenye ubora wa hali ya juu.
Mapema mwaka huu afisa mmoja ndani ya kampuni ya Samsung alitoa siri ya kwamba kampuni hiyo imeachana kabisa na utengenezaji wa kamera kwa ajili ya kuuza kutokana na kuona uhitaji wa kamera hizo ukizidi kuporomoka. Ata makampuni makubwa kama vile Nikon na Canon wapo katika hali mbaya kimauzo, mauzo yameporomoka sana.
Data hizi hapa zinaonesha jinsi gani mauzo ya kamera za kawaida (compact camera) yalivyoanza kuporomoka pale mauzo ya kamera za kutumika katika utengenezaji wa simu janja yalivyozidi kupanda.
Rangi ya njano inaashiria utengenezaji wa kamera za kutumika kwenye simu janja, rangi ya kijivu ni mauzo ya kamera ambazo si za digitali ambayo yaliyapotea kabisa. Rangi ya bluu ni ya mauzo ya kamera za kawaida – za kidigitali (Compact Digital) hasa hasa kutoka Canon na Nikon.
Ingawa Samsung wamekaa pembeni katika utengenezaji wa kamera za kawaida, yaani Compact Camera bado ni kampuni ambayo inateknolojia kubwa katika maeneo ya kamera. Tutegemee kuzidi kuona wakiongeza nguvu zao katika teknolojia za kamera kwa ajili ya simu na vifaa vingine vinavyotumia kamera.
Pia kuna wanaoamini soko la kamera za kawaida (Compact) litaendelea kuwepo ingawa litakuwa dogo, mahitaji yataendelea kuwepo hasa hasa kwa sekta ya habari.
Vipi je wewe ulishawahi kumiliki kamera ya kawaida (Compact Camera)?
Je unakubaliana na wengi ya kwamba kwa sasa ni bora kununua simu yenye kamera nzuri kuliko kutumia pesa zako katika kununua kamera za kawaida?
Vyanzo: TheInvestor, PetaPixel na tovuti mbalimbali