Kampuni nguli katika huduma za mihamala ya kifedha, MasterCard waondoa jina lao kwenye logo yao maarufu. Mkurugenzi wa kampuni amesema uamuzi huo umefanyika kama hatua ya kuonyesha ukuaji wa biashara zake kwenye nyanja mbalimbali.
Ulimwengu wa malipo yasiyotumia kadi unazidi kukua na ndiyo teknolojia inayokua kwa kasi. Ni hivi karibuni tuu MasterCard kwa kushirikiana na Vodacom waliweza kuja na bidhaa ya M-Pesa MasterCard. -> M-Pesa MasterCard
Ingawa miaka ya nyuma malipo ya kutumia kadi yalikuwa ndio kitu kikubwa zaidi kwenye biashara yao mambo yamebadilika kwa sasa. Katika ulimwengu huu wa malipo kwa njia ya mtandao, QR Code, n.k wameona hakuna umuhimu tena wa kuonyesha msisitizo kwenye sehemu ya pili katika jina lake – MasterCard, yaani Card – kadi.
Uamuzi wa kuondoa jina zima na kubakia na michoro ya duara tuu kuwakilisha kampuni hiyo umefanyika baada ya utafiti mkubwa kuendeshwa katika mataifa mbalimbali ambayo MasterCard ina biashara zake. Wamejiridhisha ya kwamba wateja wao bado wanawatambua hata bila ya neno MasterCard kuonekana kwenye nembo yao.
Katika utafiti uliofanywa kabla ya uamuzi huu kufanyika MasterCard wamesema zaidi ya asilimia 80 ya watu walioshiriki kwenye utafiti waliweza kutambua logo ya MasterCard bila uwepo wa neno la MasterCard.
Logo zisikokuwa na maneno imekuwa ni moja ya mtindo wa kisasa wa nembo za makampuni mengi. Ila sifa kubwa ni kwamba kampuni inatakiwa iwe inafahamika sana, la sivyo ni rahisi wateja kutoweza kufahamu logo husika inawakilisha kampuni gani hasa.