Kupitia maneno ya rais wa Marekani, tayari inaonekana serikali ya Marekani ipo njiani kupunguza vikwazo kwa Huawei. Inaonekana nguvu ya ushauri wa makampuni ya Marekani kwa serikali yao imeleta matunda.
Kwa kipindi kirefu tokea serikali ya Marekani chini ya Rais Trump kuweka vikwazo vya kibiashara dhidi ya Huawei kutumia bidhaa za kiteknolojia – hasa hasa vipuli muhimu katika utengenezaji wa simu na kompyuta, umoja wa makampuni mengi ya kimarekani yaliunganisha nguvu yakisihi serikali yao ibadili uamuzi huo.
Kikubwa sana ni kwamba makampuni hayo yanaamini katazo hilo la kibiashara likikaa kwa muda zaidi litasababisha Huawei kuanza kujenga mahusiano na makampuni mengine na hivyo makampuni ya Marekani kukosa kabisa soko – kumbuka Huawei ni namba mbili duniani kwenye biashara ya simu.
Pia katazo hili linaweza sababisha makampuni mengi ya China na mataifa mengine kuona ni hatari kufanya biashara na makampuni ya Marekani kwani hali kama hii ikitokea ghafla inaweza ata kuua kampuni. Mfano kampuni ya ZTE ilianza kupanda kasi na kwa mafanikio makubwa ila yote yakapotea pale ilipojikuta imewekewa vikwazo na serikali ya Marekani.
Google wao wamekuwa wakisihi serikali ya Marekani ya kwamba kwa kutotumia teknolojia za kimarekani ndio kabisa suala la uhakika wa kiusalama katika vifaa vya Huawei utapotea.
Katika mazungumzo yaliyofanyika hivi karibuni huko nchini Japani kati ya Rais wa Marekani na China yameonekana kuanza kurudisha matumaini ya biashara kati ya Huawei na makampuni ya Marekani kurudi tena – ata kama si kwa asilimia 100.
Wenyewe Huawei wamesema bado hawajapata taarifa rasmi kuhusu maneno ya Rais Trump ambayo kwenye mahojiano na waandishi wa habari alisema “….nimekubali waendelee kuwauzia baadhi ya teknolojia/bidhaa… makampuni (ya Marekani) hayakuwa yamefurahishwa na uamuzi wangu kwani wao hawaoni makosa yao kujikuta katika hali hii (ya uharibifu wa biashara zao). Hivyo nimefanya maamuzi haya (kuruhusu biashara).”
Huawei inasubiria mawasiliano rasmi kuhusu aina ya biashara ambazo zitaruhusiwa kuendelea kati yake na makampuni ya Marekani. Kumbuka kwa Marekani kampuni ya Huawei imekuwa ikitegemea toleo la Android kutoka Google, toleo la Windows kutoka Microsoft kwa ajili ya laptop. Vipuli mbalimbali vya teknolojia za ndani ya simu na kompyuta – hasa hasa chip za mawasiliano kutoka Intel Corp, Qualcomm Inc na Broadcom Corp.