Apple watambulisha MacBook Air 2018 na Mac Mini mpya. Mwezi wa tisa mwaka huu Apple walifanya utambulisho wa simu zao mpya za iPhone ila kwa tukio hili la Oktoba wamejikita zaidi katika laptop mpya, iPad na vitu vingine vidogo vidogo (gadgets).
Kwa ambao walishindwa kufuatilia tukio hilo moja kwa moja, Teknokona tunakuletea mambo makuu yaliyojiri katika tukio hilo. Kwenye makala hii zifahamu MacBook Air na Mac Mini mpya.
MacBook Air mpya – 2018
Apple wametambulisha laptop mpya ya MacBook Air ya ukubwa wa inchi 13.3
Laptop hii imekuja na ubora wa HD wa Retina display ikiwa na pixels milioni 4. MacBook Air inakelele kidogo (asilimia 17 chini) ukilinganisha na kelele za MacBook Air toleo lililopita.
Eneo la kipanya-mguso (Touchpad) limekuwa kubwa zaidi na linakuja na teknolojia ya Touch ID. Touch ID ni teknolojia ambayo tayari inatumika kwenye simu za iPhone na inawezesha simu kufunguka (unlock) kwa mguso wa kidole.
Mengineyo;
– MacBook Air mpya inauwezo wa hadi kuwa na diski uhifadhi ya ukubwa wa TB 1.5 na memori endeshaji (RAM) ya GB 16.
– Bei: Inaanzia dola 1,199 (Takribani Tsh 2,800,000/=) na kupanda kulingana na sifa.
Mac Mini mpya – 2018
Mac Mini ni kifaa kidogo cha kikompyuta. Toleo la mwanzo lilitoka miaka kadhaa nyuma na sasa Apple wameamua kuboresha zaidi kikompyuta hichi kinacholenga watu wasiopenda kuwa na CPU za ukubwa sana bila kuathiri uwezo wake wa kikazi.
Mac Mini mpya inauwezo wa kuwa na RAM (memori endeshi) ya hadi ukubwa wa GB 64. Haya ni maboresho makubwa kwani toleo la mwisho lilikuwa na uwezo wa hadi GB 16 tuu.
Mengineyo:
Bei inaanzia dola 700 (takribani Tsh 1,600,000)
Vitu vyote hivi vimetengenezwa kwa kutumia malighafi zilizokwishatumika (Recycle)
- MacBook Air, iPad Pro na Mac Mini vyote vimetengenezwa kwa kutumia malighafi zilizokwishatumika za alumini (Aluminium).
- Apple wamesema wameweza kutumia timu yao ya wahandisi kufanikisha utengenezaji wa bidhaa zao hizi mpya kutumia malighafi za alumini zilizokwishatumika kwa asilimia 100.