Ata kwenye sekta ya teknolojia huwezi kuepuka kukutana na interview za kazi unapotafuta ajira, haya ni mambo 6 muhimu kwenye interview yanayotazamwa kwenye kampuni ya Google na ambayo yanasisitizwa na makamu wa Rais wa kampuni hiyo Bi. Bonita C. Stewart.
Bi Bonita anasema wanapotafuta wafanyakazi kamapuni ya Google ina viwango vya juu katika kuangalia uelewa wa mtu juu ya aina ya kazi ataifanya, uongozi na kuwa mtu mwenye mtazamo chanya juu ya mambo mbalimbali. Bi Bonita amesema ingawa kuna vingi huwa wanaviangalia haya ni mambo sita muhimu ambayo huwa wanayatazama kwa umakini zaidi.
1. Ujuzi na Uzoefu
Anasema haijalishi aina ya kazi ambayo ameiomba, kitu kimoja muhimu wanaangalia ni je kama mtu huyo ana uzoefu na aina hiyo ya kazi.
Ata kama ajira inahitaji mtu mwenye sifa ya kuwa na Shahada ya Uzamili, kama mtu anayeomba kazi ana sifa nyingi ya uzoefu na ujuzi basi atapewa kazi hiyo ata kama hana shahada hiyo.
2. Muuliza maswali
Muuliza maswali inaonesha anataka kupata ufahamu zaidi kuhusu kazi anayoiomba au malengo ya kampuni katika eneo hilo la kazi. Lakini hapa anasisitiza maswali yasiwe marahisi ambayo majibu yake yanaweza patikana ata kupitia kutafuta Google, bali yanatakiwa yawe maswali yanayoonesha udadisi katika kufahamu mipango ya kampuni katika eneo hilo ambalo unaomba kazi.
Mfano wa maswali:
- Ni jambo gani linahitajika kufanyika katika kazi hii ambalo halifanyiki kwa sasa?
- Ni jinsi gani naweza kuwa mchango kwa kampuni nje ya majukumu ambayo yameorodheshwa kwenye tangazo la maombi ya kazi hii?
3. Wanaotaja mafanikio jumuishi
Je ukiongelea mafanikio ambayo ushawahi kuyafikia katika ajira iliyopita au ya sasa unapenda kutumia ‘Nilifanya XYZ’ au unatumia ‘Tulifanya XYZ’. Bi Bonita anasema anapenda kuajiri wafanyakazi ambao watasaidia kuwapa motisha wanaofanya kazi nao badala ya watu ambao hupenda kuchukua sifa za mafanikio peke yao.
Hii inamaanisha unapojielezea kuhusu mambo mazuri uliyofanikisha katika ajira yako ya sasa au iliyopita basi elezea katika hali ya ushirikishi na wale uliokuwa unafanya nao kazi. Kazi nyingi za siku hizi zinahitaji ushirikiano wa kuribu na wengine ili kufanikisha malengo makubwa ya kampuni/kazi husika.
4. Kubali makosa yako bila kutoa lawama
Kuweza kufanya makosa na kuwa wazi kuzungumza kuhusu makosa uliyoyafanya na kuweza kujifunza kutokana na makosa hayo ni moja ya sifa nyingine nzuri kwa ajira za sasa. Hapa anasema ni kawaida kwenye kazi makosa kutokea, anapenda kuajiri mtu ambaye atakuwa wazi kuongea kuhusu makosa yake, kuelezea alichojifunza kutokana na makosa hayo, na kuweza kuboresha utendaji wake kutokana na makosa hayo.
Anasema matatizo yatatokea tuu kwenye kazi yeyote bila kujali watu wamejiandaa vipi, mfanyakazi bora ni yule ambayo anafahamu jinsi ya kuyakubali makosa yake na kutafuta njia ya kuwa bora zaidi kwa kujifunza.
5. Kuwa na mtazamo chanya na uwezo wa kubadilika
Teknolojia zinakuwa kwa kasi sana siku hizi, na kwa namna moja au nyingine kuna jinsi ambavyo biashara zinaathirika na ukuaji huu. Biashara zinazoweza kufanikisha ni zile ambazo wafanyakazi na viongozi wake wapo tayari kubadilika kulingana na hali ya soko na teknolojia.
Anapenda kuajiri watu ambao wanaangalia mabadiliko haya na kuweza kuja na ushauri wa jinsi ya kufanya vitu tofauti. Anasema ni muhimu kwa wafanyakazi kuwa wabunifu, lakini pia wawe na uwezo wa kuwaza haraka na kuwa na uwezo wa kupokea maoni na michango ya wengine.
6. Onesha unaweza kufanya kazi vizuri na wengine
Ushirikiano ni jambo kubwa sana. Anasema kuajiri mtu mmoja mzuri ni jambo jema lakini kuwa na uwezo wa kujenga timu kwenye kampuni inayoshirikiana vizuri na kuweza kusaidiana ndio kunajenga zaidi. Mtu mmoja asiwe yeye peke yake ndio anaweza kufanya jambo flani, katika timu wafanyakazi wawe na uwezo wa kuwa rahisi kufundisha wengine na kushirikiana vizuri.
Je ni jambo gani katika haya limekugusa zaidi?
No Comment! Be the first one.