Kampuni ya Huawei imezidi kukua na sasa inatishia kuipokonya Apple nafasi ya pili katika orodha ya makampuni yanayoingiza sokoni simu nyingi zaidi.
Kwa muda mrefu sasa nafasi ya kwanza imekuwa ikishikiliwa na Samsung, kufuatiwa na Apple na Huawei imekuwa inashika nafasi ya tatu. Ila uporomokaji wa mauzo ya simu za iPhone imeifanya Apple kupunguza idadi ya simu inazotengeneza ukilinganisha na kipindi cha mwaka 2015.
Huawei wanamiaka chini ya 5 katika biashara ya utengenezaji simu…na tayari wamewaacha mbali Sony, HTC na LG – makampuni ambayo yalikuwa juu zaidi yao katika biashara hiyo. Ndani ya miezi 12 kuna uwezekano mkubwa Huawei wakaipokonya Apple nafasi ya pili.
Ni siku chache tuu zilizopita tayari Huawei wametambulisha simu janja ya kiwango cha juu cha ubora na inaonekana simu hiyo, Huawei Mate 9, itaweza nufaika kutokana na majanga ya Samsung Galaxy Note 7 na hivyo kuuzika vizuri zaidi. Simu hii ya Huawei ikifanya vizuri sokoni basi kuna uwezekano mkubwa sana miezi michache ijayo Huawei watanyakua nafasi ya pili kutoka Apple kwani tayari wamewabana kwelikweli.
Kutokuwepo kwa simu za Galaxy Note 7 sokoni kunamaanisha simu yao mpya ya Huawei Mate 9 haitapata ushindani mkubwa sokoni kwenye simu za ukubwa wa inchi 5.5 na zaidi..
Na pia ingawa kwa muda mrefu Huawei wamekuwa wanatumia kiasi kidogo cha pesa kwenye matangazo (marketing & advertising) kwa kipindi hichi wamezidi kuongeza bajeti katika eneo hilo.
Mjumlisho wa utumiaji wa pesa nyingi zaidi kwenye kujitangaza pamoja na uletwaji wa simu janja za kiwango cha juu zinazokubalika katika masoko ya Ulaya na Marekani kunaiweka Huawei katika nafasi nzuri zaidi kimafanikio kimauzo.