Unapotembelea makaburi yoyote pale katika nchi mbalimbali duniani lazima utakutana na kibao maalumu kinachoandikwa jina la marehemu, tarehe ya kuzaliwa na kufariki kwake.
Wakati mwingine waweza kukuta jina ambalo linafanana na mtu uliyewahi kumfahamu lakini huna hakika ndiye au ni mfanano wa majina.
Lakini kwa msaada wa ukuaji wa kasi wa teknolojia sasa utaweza kuona picha za marehemu na video za wakati wa uhai wake pindi tu utakapo lisogelea kaburi lake.
Aidha pia kunawekwa hitoria yake kwa njia ya maandishi kwa urefu utakao hata kama ni maandishi
yatakayotengeneza kitabu cha riwaya.
Jiwe la kiditali la kaburi hilo linafanya kazi kama simu za kisasa aina ya Smartphone. Kwa mbali unaweza kuona kama ni sawa na makaburi mengine, huonesha jina la marehemu, tarehe ya kuzaliwa na kufa.
Lakini ukilikaribia linapata uhai. Kuna sensor maalum ambayo mtu anapolikaribia kaburi hilo huanza kuonesha picha za marehemu na maelezo yote yaliyowekwa yanayomuhusu.
Watengenezaji wa makaburi hayo ya kidigitali wanasema njia ya hii ya kucheza picha pindi awepo mtu karibu husaidia kutunza nishati ya umeme kwa muda mrefu zaidi.
Saso Radovanovic, mkuu wa kampuni ya Bioenergija inayotengeneza makaburi hayo anasema tayari ameshapata oda chache kutoka wateja kadhaa wanaohitaji aina hiyo ya makaburi.
Kwa anayehitaji anasema itamgharimu takriban euro Elfu tatu sawa na Tsh Milioni Saba na Nusu. Pia ameongeza kusema wataboresha zaidi kwa kuwezesha kusikika sauti za video zitakazoonekana kwenye kaburi kupitia simu janja ya mtu aliyekuja kaburini ili kuepusha kelele pindi sauti itakapotoka katika kaburi la kidigitali.